TAMKO LA MTANDAO WA WATETEZI
WA HAKI ZA BINADAMU KUITAKA SERIKALI KULIFUNGULIWA GAZETI LA MWANAHALISI
Ndugu wanahabari: Ninyi ni mashahidi wa
jinsi ambavyo Serikali ya Jamhuri ya Muungano imekuwa ikijitangaza kwaba
inasimamia misingi ya utawala bora nchini. Lakini ninyi nyote mmeshuhudia
ambavyo serikali hii imeshindwa
kusimamia utawala wa sheria na kuzilinda haki za binadamu.
Majigambo ya serikali kwamba inaheshimu na kusimamia
misingi ya demokrasia na utawala bora hayaendani na ukweli halisi. Na hivi
sasa, dunia imeanza kushuhudia kuwa wimbo huu unaoimbwa na kuchezwa na serikali
hauna ukweli wowote.
Hii ni kwa sababu, leo ni siku ya 175 tangu serikali
itangaze kulifungia “kwa muda usiojulikana,” gazeti la kila wiki la
MwanaHALISI. Kipindi hiki ni sawa na miezi mitano na siku 24 au miezi sita
kasoro siku tano. Huu ni nusu mwaka. Tangu 30 Julai 2012, ilipotangazwa
kufungiwa kwa gazeti hilo, wadau wa habari na wananchi wengine kwa ujumla wao;
wamekuwa wakipaza sauti kuiomba serikali kulifungulia Mwanahalisi gazeti
kipenzi cha wananchi, lakini serikali imekuwa kimya.
Kufungiwa kwa gazeti la Mwanahalisi kulitokana na
taarifa ambazo zilikuwa na mvuto wa kipekee kuhusiana na kutekwa, kuteswa na
kisha kutupwa katika msitu wa Mabwepande, Mwenyekiti wa Jumuiya ya Madaktari
nchini Dk. Stephen Ulimboka ambaye aliwaongoza madaktari nchini katika kudai
maslahi bora, vitendea kazi pamoja na mazingira bora ya kazi.
Masuala kama haya ya kumteka, kumtesa na kumtupa Dk.
Ulimboka msituni; na kumfanya nusu mfu; kulifungia gazeti la Mwanahalisi,
kuuawa kikatili kwa bomu kwa mwandishi wa kituo cha televisheni cha Chanel Ten,
Daudi Mwangosi, kutishiwa kwa watetezi wa haki na mengine mengi, ndiyo
yanayotikisa dunia hivi sasa.
Sisi tunaihoji serikali ni lini italifungulia gazeti
hili ili wasomaji wake wapate haki yao ya kikatiba ya kupata habari bila
kuzuizi? Ni lini serikali itakuwa na huruma na wafanyakazi wa Hali Halisi
Publishers Limited, inayochapisha gazeti hili ili kupunguza wimbi la waliokosa
ajira nchini?
Kwa namna yoyote ile hakuna taifa linaloweza kusema
linapinga ukandamizaji wa uhuru wa kupata habari na kutaka liheshimiwe katika
jamii ya kimataifa wakati taifa hilo linaendeleza ukandamizaji wa haki nchini
mwake. Tunasema hivyo kwa sababu miongoni mwa viashiria vikuu vya udikteta
popote duniani ni pamoja na kuminya uhuru wa vyombo vya habari, na kuwatishia
wanaharakati wanapodai haki za raia dhidi ya ukiukwaji wa haki unaofumbiwa na macho na serikali iliyoko
madarakani.
Ndugu waandishi wa habari: Kutokana na mazingira hayo,
sisi wanamtandao wa watetezi wa haki za binadamu, chini ya mwamvuli wa Tanzania
Human Rights Defenders (THRD-Coalition) tunaisihi tena serikali kuurejea uamuzi
wake na kulifungulia gazeti la Mwanahalisi. Msimamo huu si wa kikundi fulani bali wa
mtandao mzima ambao ni kusanyiko la zaidi ya asasi 60 za kiraia na kwa
kushirikiana bega kwa bega na mwanachama mwanzilishi na mwakilishi wa Taasisi
ya vyombo vya habari Kusini mwa Afrika – Tawi la Tanzania (MISA TAN) tunarejea
wito wetu wa kuisihi serikali ilifungulie mara moja gazeti la Mwanahalisi na
bila masharti.
Leo tunatoa wito huu, tukiwa
na sababu za nyongeza, nazo ni kama ifuatavyo:
Kwanza, Mkuu wa Jeshi la Polisi nchini, IGP Said Mwema
amekiri mbele ya wanahabari kuwa kutekwa na kuteswa kwa kiongozi wa Jumuiya ya
Madaktari nchini, Dkt. Steven Ulimboka, “Ni siri ya Taifa.” Je, ina maana kuwa kuwa uhai wa Dkt. Ulimboka
ni siri ya Taifa? Na je serikali imemkabidhi nani jukukumu lake la msingi la
kulinda watetezi wa haki za binadamu kama vyombo husika vinatupiana mpira?
Ndugu wanahabari: Ninyi mnajua kuwa kufungiwa kwa
gazeti la MwanaHALISI kulitokana na kuanika kwa ushahidi mwanana usiotia shaka juu
ya wanaotajwa kuhusika na utekaji na utesaji wa kiongozi huyo. Aidha, kufungiwa
kwa MwanaHALISI kulifuatia hatua ya gazeti kumtaja Bw. Ramadhani Ighondu, kuwa
ndiye aliyehusika na kupanga njama za kumteka na kumtesa Dkt. Ulimboka. Lakini
hili pia limethibitishwa na hata Dkt.
Ulimboka mwenyewe wakati alipokuwa katika hospitali ya Muhimbili na baadaye
aliporejea nchini katika tamko lake lililosomwa na wakili wake.
Hatua ya IGP Mwema kusema suala la kutekwa kwa Dkt.
Ulimboka ni “siri ya taifa” na hatua ya Kamanda wa Kanda Maalum ya Dar es
Salaam, Sulemain Kova kusema “suala la Ulimboka lipo mikononi mwa wakubwa
wangu,” yanathibitisha uchunguzi wa MwanaHALISI ulikuwa sahihi.
Ndugu wanahabari: Kutokana na
maelezo hayo hapo juu sasa tunaitanabahisha serikali kwa yafuatayo:
a) Rais Kikwete aingilie kati suala hilo kwa
sababu, Waziri Mkuu Mizengo Kayanza Peter Pinda, aliliambia Bunge mjini Dodoma,
tarehe 16 Agosti 2012, kwamba “suala la kufungiwa kwa MwanaHALISI liko kwenye
mamlaka ya juu ya nchi”
Waziri Mkuu alisema, “Kama kuna mtu yoyote
asiyeridhika na uamuzi wa kulifungia gazeti la MwanaHALISI akate rufaa katika
mamlaka ya juu.” Waziri Mkuu hakusema, MwanaHALISI
waende mahakamani. Alitaja
mamlaka ya juu, na kwamba mamlaka ya juu ya Waziri Mkuu hayawezi kuwa waziri wa
habari. Mamlaka ya juu ya Waziri Mkuu ni Rais.
Uamuzi huo wa rais utalisaidia taifa kurejesha heshima na haiba ambayo
sasa imetoweka kutokana na uvunjifu wa wazi wa haki za binadamu.
b) Tunataka hili lifanyike sasa kwa sababu,
tumepata taarifa kuwa serikali iko mbioni kupeleka muswaada wa sheria ya huduma
za vyombo vya habari bungeni bila kuwa na muswada wa sheria ya kupata habari.
Sisi tunajiuliza, unawezaje kupeleka mswaada huo, wakati hapohapo, serikali
hiyohiyo imelifungia gazeti. Hivyo basi,tunaitaka serikali kabla ya kupeleka
mswaada bungeni, kufuta sheria inayokandamiza uhuru wa habari yaani Newspaper
Act 1976 - ambayo imetumika kulifungia gazeti la Mwanahalisi na kwa maana hiyo
inaweza kuyafungia hata mengine.
Kwa kuwa serikali ya Rais Kikwete imekuwa
ikitajwa kuwa ni sikivu tunamsihi asikilize kilio cha watanzania na kuagiza watendaji wake walifungulie gazeti
hili kipenzi cha wote mapema
iwezekanavyo.
......................................
Tumaani Mwailenge,
Mkurugenzi Mtendaji-
MISA-Tan.
Onesmo Olengurumwa-
Mratibu wa Kitaifa THRD-Coalition
0 comments:
Post a Comment