Mkurugenzi wa Mikopo na Biashara wa
TADB, Bw. Robert Paschal (aliyesimama) akihutubia wakulima wadogo zaidi ya
340 (hawapo pichani) wa mkoa wa Morogoro wakati warsha ya wakulima wadogo zaidi
ya 340 wa Mkoa wa morogoro iliyofanyika katika Ukumbi wa Mazingira Halmashauri
ya Wilaya ya Kilombero. Kulia ni Mkuu
wa Wilaya ya Kilombero, Mhe. Lephy Gembe.
Mkuu wa Wilaya ya Kilombero, Mhe. Lephy Gembe (aliyesimama) akihutubia wakulima wadogo zaidi ya
340 (hawapo pichani) wa mkoa wa Morogoro wakati warsha ya wakulima wadogo zaidi
ya 340 wa Mkoa wa morogoro iliyofanyika katika Ukumbi wa Mazingira Halmashauri
ya Wilaya ya Kilombero. Kushoto Mkurugenzi wa Mikopo na Biashara wa TADB, Bw.
Robert Paschal.
Mkuu wa Wilaya ya
Kilombero, Mhe. Lephy Gembe (Wapili
kushoto) akizungumza na Mkurugenzi wa Mikopo na Biashara wa TADB, Bw. Robert
Paschal (Wapili kulia)
Picha ya pamoja
Mkurugenzi wa Mikopo na Biashara wa
TADB, Bw. Robert Paschal (aliyesimama) akihutubia mkutano huo wa wakulima wadogo
Na
Mwandishi Wetu
Wakulima wa zao la mpunga
wanaojishughulisha na kilimo cha umwagiliaji katika Kijiji cha Mkula wilayani
Kilombero mkoa wa Morogoro wamefanikiwa
kupata mkopo wa shilingi Milioni 890 kutoka Benki ya Maendeleo ya Kilimo Tanzania
(TADB) ili kuongeza
tija na uzalishaji wa zao la mpunga.
Hayo yaliwekwa bayana na Mkurugenzi
wa Mikopo na Biashara wa TADB, Bw. Robert Paschal wakati wa warsha ya wakulima
wadogo zaidi ya 340 wa Mkoa wa morogoro iliyofanyika katika Ukumbi wa Mazingira
Halmashauri ya Wilaya ya Kilombero.
Bw. Paschal alisema lengo la mkopo
huo unaowanufaisha zaidi ya wakulima 350 ni kuongeza tija na uzalishaji wa
mpunga ili Kusaidia upatikanaji wa utoshelezi na usalama wa chakula ambao ni
endelevu nchini Tanzania na kuchagiza na kusaidia Mapinduzi
ya Kilimo kutoka kilimo cha kujikimu kwenda cha
kibiashara ili kuchangia kwenye ukuaji wa uchumi na kupunguza umaskini.
“Mkopo huu na mengine tunayotoa imelenga
kuongeza tija na uzalishaji katika kilimo ili kusaidia kukabiliana na mapungufu
hayo na kuhuisha upatikanaji wa mikopo katika sekta ya kilimo ili kuleta
mapinduzi katika kilimo nchini,” alisema Bw.
Paschal.
Kwa mujibu wa Bw. Paschal mkopo
huo utasaidia shughuli mbalimbali za utayarishaji wa mashamba, kupima ubora wa
udongo na virutubisho vinavyohitajika kwenye uzalishaji wa mpunga pamoja na
kuwezesha upatikanaji wa pembejeo za kilimo zikiwemo mbegu bora, mbolea na
madawa.
Mkurugenzi huyo aliongeza kuwa
Benki imetoa mkopo kwa ajili ya uwekezaji kwenye ujenzi viwanda vya kusindika
mazao, ununuzi wa mitambo na ufungaji wa mitambo ya usindikaji wa mpunga ili
kuongeza thamani wa zao hilo.
“Tunaamini
mkopo huu utachagiza kuongezeka kwa upatikanaji wa chakula
na Pato la Taifa kutokana kuongezeka kwa tija na uzalishaji hivyo kuwa chachu
ya ongezeko la thamani, ukuaji wa viwanda vya mazao ya kilimo hivyo kuchangia
kuongezeka kwa ajira nchini,” aliongeza.
Akizungumzia mikakati ya TADB kwa sasa, Bw. Paschal alisema Benki
imejipanga kutoa mikopo ya Muda Mfupi, Mikopo ya Muda wa Kati na Mikopo ya Muda
Mrefu kwa kutumia njia mbalimbali. Mbinu hizo zinajumuisha pamoja na mambo
mengine; mikopo ya moja kwa moja kwa vikundi vya wakulima wadogo wadogo; kutoa
mikopo kwa njia ya marejesho taasisi zinazokopesha; utoaji wa mikopo kwa pamoja
na kushirikiana na taasisi/benki zingine; pamoja na mikopo ya miundombinu
inayolenga kupunguza mapengo ya upatikanaji wa fedha katika minyororo ya
ongezeko la thamani ya kipaumbele.
“Kwa kuanzia, TADB imelenga uwekezaji katika maeneo nane (8) ya
minyororo ya uongezaji wa thamani ambayo ni: nafaka, kilimo cha mboga mboga,
kilimo cha bidhaa za viwanda, mbegu za mafuta, ufugaji wa ng’ombe, ufugaji
kuku, ufugaji wa samaki na bidhaa za misitu. Benki pia inajitahidi kusimamia
fedha kutoka kwa wafadhili wengine ambazo zimeelekzwa kwenye kuendeleza
kilimo,” alisema.
0 comments:
Post a Comment