Tuesday, June 14, 2016

SERIKALI YATANGAZA UTARATIBU MPYA MAADHIMISHO YA WIKI YA UTUMISHI WA UMMA, PIA YAFAFANUA FEDHA ZILIZOOKOLEWA WATUMISHI HEWA.

Na. Aron Msigwa –MAELEZO.
 Dar es salaam.

SERIKALI imetangaza utaratibu mpya utakaofuatwa wakati wa Maadhimisho ya Wiki ya Utumishi wa Umma kuanzia Juni 16 hadi 23, 2016 ambapo imewaagiza Watendaji Wakuu katika Wizara, Idara zinazojitegemea, Wakala na Taasisi za Serikali kutenga siku moja ya kukutana na watumishi katika sehemu zao za kazi kwa lengo la kusikiliza kero mbalimbali zinazowakabili na kuzitafutia ufumbuzi.

Aidha, imewaagiza watendaji hao kutenga siku nyingine moja kwa ajili ya kukutana na wananchi, kusikiliza na kuzitafutia ufumbuzi kero zao zinazohusiana na huduma zinazotolewa na Taasisi zao.

Akitangaza utaratibu huo leo jijini Dar es salaam Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma Mhe. Angellah Kairuki amesema kuwa Serikali imeamua kubadili mfumo wa maadhimisho hayo kwa lengo la kuongeza ushiriki wa wananchi na watumishi wa umma katika maadhimisho hayo.

Ameongeza kuwa wakati wa maadhimisho hayo Watendaji hao watatakiwa kukutana wananchi na kusikiliza kero zinazohusiana na huduma zinazotolewa na taasisi zao pia kukutana na watumishi wa umma katika sehemu zao za kazi kusikiliza kwa lengo la kusikiliza kero zinazowakabili zikiwemo za upandishwaji wa vyeo, madai mbalimbali na taratibu mbalimbali kuhusu utumishi wa umma.

Amesema kuwa baada ya maadhimisho hayo kila Wizara, Mamlaka ya Serikali za Mitaa na Taasisi ya Umma itapaswa kuandaa taarifa jinsi ilivyotekeleza maagizo yaliyotolewa kwa kuiwasilisha Ofisi ya Rais, Utumishi wa Umma kabla ya Juni 30, 2016.

Ameeleza kuwa Tanzania inaungana na mataifa mengine ya Bara la Afrika kuadhimisha Wiki ya Utumishi wa Umma Barani Afrika  chini ya Kaulimbiu isemayo Uongozi wa Umma kwa Ukuaji Jumuishi:kuelekea katika Afrika tunayoitaka.

Mhe. Angellah amebainisha kuwa maadhimisho ya mwaka huu yatajikita katika kuangalia mchango wa Utumishi wa Umma katika ukuaji wa uchumi Barani Afrika, mchango wa Utumishi wa Umma katika kuiwezesha Ajenda ya Afrika ya 20163 ambayo inaweka mkazo katika maendeleo ya Afrika na Haki za Wanawake.

Amesisitiza kuwa malengo na mkakati wa Serikali ya awamu ya tano ni kufikia uchumi wa viwanda uliofungamanishwa na maendeleo ya watu, Tanzania ikiwa imejiwekea malengo ya kupiga hatua katika ukuaji wa uchumi kupitia maendeleo ya viwanda.

Amesema ili kufikia azma hiyo Serikali kupitia Utumishi wa Umma ina wajibu wa kuwawezesha wananchi kushiriki katika shughuli za uzalishaji ili kukuza uchumi huku watumishi wa umma wakitakiwa kufanya kazi kwa bidii, maarifa na weledi, kutoa huduma kwa wananchi wote kwa wakati pasipo urasimu wala ukiritimba pia kuepuka vitendo vya rushwa katika utekelezaji wa majukumu yao.

“Katika hili Watumishi wa umma lazima wawe na utendaji unaoweza kupimika, ili kulitekeleza hili kuanzia tarehe 1 Julai tutaanzisha dhana ya mfumo wa utendaji wa taasisi mbalimbali kwa lengo la kupima utendaji wa taasisi kulingana na matokeo tunayoyapata” Amesisitiza.

Ameongeza kuwa watumishi wa umma Serikalini wanatakiwa kuwa na utendaji unaojali matokeo, kuepuka vitendo vya wizi, ufisadi na udanganyifu vinavyosababisha upotevu wa fedha za Serikali.
Akizungumza kuhusu Haki za Wanawake katika utumishi wa umma amesema kuwa Serikali itaendelea kuhakikisha kuwa  kuna uwiano wa jinsia katika nafasi na fursa mbalimbali katika ajira , Uteuzi wa nafasi za uongozi , mafunzo kazini na upandishwaji vyeo.

UFAFANUZI KUHUSU WATUMISHI HEWA.

Kuhusu suala la kuwaondoa Watumishi hewa katika orodha ya malipo ya Serikali  Mhe. Angellah amefafanua kuwa tayari Ofisi yake imekwishatoa maelekezo kwa Makatibu Wakuu, Wakuu wa Taasisi zote za Umma pamoja na Mamlaka za Serikali za Mitaa yanayowataka kuwasilisha taarifa ya mwisho ya watumishi hewa ifikapo Juni 15, 2016.

Amesema taarifa itakayowasilishwa itatakiwa kubainisha majina , namba za utambulisho wa watumishi hewa/ cheki namba, tarehe waliyotakiwa kuondolewa kwenye mfumo wa malipo na kiasi kilichopotea  na kile kilichookolewa ikiwa imesainiwa na Mkuu wa Wizara, Mamlaka ya Serikali za Mitaa na Taasisi husika.
Ameeleza kuwa mara baada ya kuzipokea taarifa hizo Serikali itazifanyia tathmini ili kupata uhakika wa zoezi zima la kuondoa watumishi hao kuanzia kuanzia tarehe 15 Machi 2016.

“Kama mmekuwa mkifuatilia taarifa mbalimbali Serikali tumekuwa tukilishughulikia kwa nguvu suala hili la watumishi hewa kuanzia mwezi Machi mwaka huu  Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli alipotoa maagizo ya kuwaondoa watumishi hewa katika orodha ya malipo ya Serikali” Ameeleza.
Aidha, amebainisha kuwa kuwa kuanzia Machi, 1, 2016 hadi Mei 30, 2016 watumishi 12,246 wameondolewa kwenye mfumo wa malipo ya mishahara kwa sababu mbalimbali zikiwemo za kutimiza umri wa kustaafu kwa lazima au kufukuzwa kazi ,vifo,kuhitimishwa kwa mikataba na ugonjwa.

Jumla ya shilingi 25,091,292,688.82 zingepotea kama watumishi hao wasingeondolewa kwenye mfumo wa malipo ikilinganishwa na watumishi 10,295 walioondolewa kwenye mfumo hadi Aprili 30, 201 huku kiasi kilichookolewa kikifikia shilingi 23,206,547,598.82 likiwa ni ongezeko la watumishi 1,951 na shilingi 1,884,745,090.

MWISHO.
Share this article :

0 comments:

Post a Comment

 
MZUKA BLOG © Copyright 2014. All Rights Reserved.

Powered by MATERU FROM IBS.
imagem-logoRudi Juu