Na
Jacquiline Mrisho - MAELEZO Kigoma
Kambi ya
wakimbizi ya Nduta iliyopo wilayani Kibondo Mkoa wa Kigoma imewatengea eneo
maalumu la kuishi watu wenye ulemavu wa ngozi ili kulinda usalama wa maisha
yao.
Hayo
yamesemwa na Mkuu wa Kambi hiyo, Peter Buluku alipokuwa akiongea na mwandishi
wa habari hii juu ya maisha halisi ya wakimbizi hao wanaoishi katika kambi hiyo
wakitokea nchini Burundi.
Buluku amesema
kuwa katika kambi hiyo kuna baadhi ya wakimbizi wanaojihusisha na vitendo
vinavyohatarisha usalama wa wakimbizi wenzao vikiwemo vya ubakaji, wizi na kujaribu
kuteka watu wenye ulemavu wa ngozi.
Mkuu huyo
wa kambi amefafanua kuwa mnamo mwezi Aprili mwaka huu, familia moja yenye mtoto
mwenye ulemavu wa ngozi ilivamiwa na watu wasiojulikana na kumchukua mtoto huyo
lakini kwa bahati nzuri majirani walijitahidi kupiga kelele hivyo, watuhumiwa
waliamua kumtelekeza mtoto huyo na kukimbilia kusikojulikana.
"Kutokana
na kujitokeza kwa hali hiyo, Sisi pamoja na Mashirika yasiyo ya Kiserikali yanayotoa huduma kambini hapa tuliamua
kuwatengea eneo maalumu lililo karibu na kituo cha polisi watu hawa wenye ulemavu
wa ngozi ili wawe na ulinzi wa kutosha hivyo kuishi kwa amani kama binadamu
wengine", alisema Buluku.
Hadi sasa kambi
hiyo ina jumla ya watu watano wenye ulemavu wa ngozi kutoka kwenye familia
mbili tofauti, Shirika la kuhudumia wakimbizi duniani (UNHCR) limehaidi kujenga
jengo la kudumu kwa ajili ya watu wenye ulemavu huo.
Kambi ya
Nduta ilianzishwa rasmi mwaka 1998 na kufungwa mwaka 2009. Ilifunguliwa kwa mara
ya pili mwaka 2015 baada ya kutokea kwa vurugu nchini Burundi na kusababisha
baadhi ya raia wa nchi hiyo kukimbilia nchini Tanzania, hadi sasa kambi hiyo
ina jumla ya wakimbizi 55,320 ambao ni raia
wa Burundi.
0 comments:
Post a Comment