Monday, July 18, 2016

VODACOM YAFANIKISHA MAWASILIANO KATIKA SAFARI YA KUPANDA MLIMA KILIMANJAR


Mkuu wa Vodacom Kanda ya Kaskazini,Henry Tsamburakis akizungumza na wageni raia wa Afrika Kusini  wanaopanada Mlima Kilimanjaro kwa lengo la kuchangisha fedha za kununua taulo za watoto wa kike wawapo katika siku zao za Hedhi.
Mkuu wa Vodacom Kanda ya Kaskazini,Henry Tsamburakis akimsaidia mmoja wa wageni hao kubadili lugha ya kiswahili katika simu yake kwenda ya Kiingereza.
Wageni wakipiga Selfie kabla ya kuanza safari yakuelekea lango la Marangu kwa ajili ya kupanda mlima Kilimanjaro.
Raia wa Afrika Kusini wanaopanda Mlima Kilimanjaro kwa ajili ya kuchangisha fedha za kunua taulo za watoto  wa kike  pamoja na kusherehekea kumbukumbu ya kuzaliwa kwa baba wa taifa la Afrika Kusini ,Nelson Mandela.
Baadhi ya wapagazi katika Mlima Kilimanjaro wakishusha mabegi ya wageni hao kabla ya kuanza safari ya kupanda mlima Kilimanjaro.
Baadhi ya wageni wakihakiki mabegi yao.
Baadhi ya wageni wakiwasili katika lango la Marangu tayari kuanza changamoto ya kupanda Mlima Kilimanjaro.
Wapagazi katika Mlima Kilimanjaro wakiwa katika foleni ya kupima uzito mizigo yao.
Wageni wakijiandikisha kabla ya kuanza safari ya kupanda Mlima Kilimanjaro.
Mkuu wa Vodacom Kanda ya Kaskazini akizungumza na mmoja wa viongozi wa wageni hao ,Gerry Elsdon kabla ya kuanza safari ya kupanda Mlima Kilimanjaro.
Kiongozi wa ugeni kutoka Afrika Kusini ,Richard Mabaso akizungumza kabla ya kuanza safari hiyo.
Wageni kutoka Afrika Kusini wakiwa katika picha ya pamoja na Mkuu wa Vodacom Kanda ya Kaskazini,Henry Tsamburakis muda mchache kabla ya kuanza kupanda mlima Kilimanjaro.
Safari ya kuanza kupanda Mlima Kilimnjaro ikaanza.
Na Dixon Busagaga wa Michuzi Blog ,Kanda ya Kaskazini.

 KAMPUNI ya mawasiliano ya simu za mkononi ya Vodacom Tanzania imedhamini safari ya siku sita kwa raia 36 wa Afrika Kusini wakiwemo wafanyakazi wa kampuni hiyo, kupanda Mlima Kilimanjaro yenye lengo la kuchangisha pesa kwa ajili ya Taulo za watoto wa kike.

Kampuni ya Vodacom inadhamini safari hiyo ambayo hufanyika kila mwaka kama sehemu ya kumbukumbu ya kuzaliwa kwa muasisi wa Taifa la Afrika Kusini, Hayati Nelson Mandela, ikiwa ni mara ya pili mfululizo kwa Vodacom kufanya hivyo.

Akizungumza wakati wa kuanza changamoto ya kupanda mlima Kilimanjaro kwa kundi hilo la watu 36,Mkuu wa Vodacom kanda ya Kaskazini, Henry Tsamburakis alisema Vodacom imetoa mawasiliano wakati wote wa safari ya kupanda mlima ili wasipate tatizo la kushindwa kuwasiliana na ndugu zao pamoja na kutuma picha za matukio wawapo mlimani.

"Vodacom Tanzania tunajivunia kuweza kuwadhamini watalii na baadhi ya wafanyakazi wa Vodacom kutoka Afrika ya kusini kwa mwaka wa pili mfululizo kwa kudhamini Mfuko wa Mandela ambapo kila mwaka watalii hawa huja nchini mwetu mwezi wa saba  kupanda mlima wa Kilimanjaro wakiwa na lengo la kuchangisha pesa kwa ajili ya  kusaidia watoto wa kike" alisema Tsamburakis. 

"Kwa upande wetu Vodacom Tanzania tumeamua kuwapatia udhamini wa mawasiliano ili wasipate matatizo ya mawasiliano wakiwa katika harakati za kupanda mlima Kilimanjaro waweze kutuma picha au kuwasiliana na ndugu zao kwa urahisi zaidi kupitia 4G yetu,"aliongeza Tsamburakis. 

Alisema Vodacom imetoa vifaa maalumu (Routers) sita  zikiwa zimeunganishiwa katika mtandao wa kasi huku zikiwa zimewekewa bando ya GB 10 watakazoweza kutumia kwa muda wote watakapokuwa mlimani. 

Akizungumza kwa niaba ya wenzake, Gerry Elsdon ameishukuru kampuni ya Vodacom kwa kuwezesha mawasiliano hatua itakayochangia safari yao ya kuelekea katika kelele cha Uhuru katika mlima Kilimanjaro kuwa rahisi zaidi. 

"Niishukuru kampuni ya Vodacom kwa niaba ya wenzangu, imewezesha mawasiliano yetu kuwa rahisi sasa,kwa sababu tuliamini kuwa tutakua nje ya mawasiliano kwa zaidi ya siku sita kumbe sasa tutaendelea kuwasiliana na ndugu na jamaa" alisema Elsdon.

Kwa upande wake mratibu wa safari hiyo ambayo hujulikana kama Treck4mandela,Richard Mabaso alisema lengo la safari hiyo ni kuendelea kuchangisha fedha kwa ajili ya kununua Taulo za kike kwa watoto wa kike wasio na uwezo ili kukitumia pindi wawapo katika siku za hedhi.

""Tunatambua changamoto zinazowakabili watoto wa kike hasa wale walioko mashuleni pindi wanapoingia katika siku zao,kupitia Mfuko wa Mandela tumeendelea kuchangisha pesa kwa ajili ya kuwasaidia angalau kupata Taulo ili waweze kuendelea na masomo bila ya kuwa na kikwazo." alisema Mabaso.

Alisema mbali na zoezi hilo kulenga kuchangisha fedha kwa ajili ya watoto wa kike pia limekua likitumika kusherehekea kumbukumbu ya kuzaliwa kwa baba wa Taifa la Afrika Kusini, Nelson Mandela.

Share this article :

0 comments:

Post a Comment

 
MZUKA BLOG © Copyright 2014. All Rights Reserved.

Powered by MATERU FROM IBS.
imagem-logoRudi Juu