Waziri Nape Nnauye
azindua Miradi Nane inayofadhiliwa na Tanzania Media Foundation.
Na Benedict Liwenga,
WHUSM.
Serikali kwa kushirikiana na Uongozi wa Tanzania Media
Foundation itaendelea kushirikiana bega kwa bega katika kuwawezesha Waandishi
wa Habari nchini kupenda kutembelea maeneo ya vijijini na kuandika habari
mbalimbali kuhusu changamoto za maeneo hayo.
Kauli hiyo imetolewa leo na Waziri wa Habari, Utamaduni,
Sanaa na Michezo, Mhe. Nape Nnauye wakati akizindua Miradi Nane ambayo inafadhiliwa
na Taasisi hiyo ambayo unahusisha Waaandishi wa Habari kutembelea maeneo ya
vijijini na kuandika habari mbalimbali kwa lengo la kuelimisha Umma.
Mhe. Nnauye amesema kuwa, Serikali inatambua mchango mkubwa
unaofanywa na Taasisi hiyo ya kuwajengea uwezo Waandishi wa habari na
kuwawezesha kifedha kwa ajili ya kwenda kutafuta habari mbalimbali katika
maeneo ya vijijini.
‘’Ni muhimu kwa waandishi wa habari kufika maeneo ya vijijini
na kuapata habari mbalimbali kwa jili ya kuhabarisha umma, hivyo Serikali bado
iko na nyie na itaendelea kuwaunga mkono na endeleeni na kazi hiyo nzuri’’,
alisema Mhe. Nnauye.
Ameongeza kuwa, kuna haja ya Taasisi hiyo kuendelea kujenga
uwezo wa kusaidia kupata umakini katika kazi za habari ili jamii iweze kuwa na
imani na Serikali pamoja na Vyombo vya habari na pia kuonyesha juhudi ya
kuendelea kuwajengea uwezo wanahabari ili waweze kuwafikia watu wenye mahitaji
makubwa ya habari ambao ni watu wa vijijjini ambao wakati mwingi wamekuwa
wakichelewa kupata habari.
Kwa upande wake Mkurugenzi wa Tanzania Media Foundation, Bw.
Ernest Sungura ameyataja baadhi ya mafanikio yaliyofikiwa na Taasisi hiyo
katika kuwajengea uwezo wanahabari nchini ambapo amesema kuwa, mpaka sasa
wameweza kuwajengea uwezo jumla ya Waandishi wa habari wapatao 700 pamoja na
Vyombo vya Habari 135.
Mbali na kuanza na miradi ya mwandishi mmoja mmoja, kwa sasa
wanatarajia kuanza na miradi mingine inayoanza mwishoni mwa mwezi huu na
itakuwa ni ya Awamu ya Pili ambapo itahusisha jumla ya Waandishi wa habari
wapatao 30 kwenda vijijini kufanya kazi za kihabari na kupewa mafunzo ya namna
ya kuandika habari za vijijini.
‘’Kwa sasa tumeanza mradi wa watu kubobea katika eneo maalum na safari hii tutajikita katika masuala
ya Viwanda yaani kuwaandaa waandishi wa habari watakaobobea katika masuala ya
viwanda na tayari tumeshamdokeza Waziri wa Viwanda kuhusu taarifa hizo kwa
ajili ya kuizindua miradi hiyo’’, alisema Sungura.
Ameongeza kuwa katika kuandika masuala ya viwanda, tayari
kuna waandishi wa habari wapatao 10 ambao hivi sasa wanajengewa uwezo ili waweze
kuendana na kasi ya Serikali na katika suala la kuwandaa waandishi hao wanatumia
Waandishi wa habari wazoefu pamoja na wadau wengine.
Amefafanua kuwa, lengo kubwa la kazi hizo zote ni kuwawezesha
waandishi nchini kuweza kuyafikia maeneo ambayo yamekuwa hayafikiki, hivyo
wanatoa rasimali fedha kwa waandshi hao ili kuweza kutembelea maeneo hayo na kuhabarisha
umma.
‘’Ziko takwimu nyingi kila mahali kama vile za maji, afya,
alimu lakini baadhi ya waandishi wetu hawafanyi ule uandishi wa kuzifanya takwimu
hizo zieleweke na ziwe na manufaa kwa walaji, hivyo sisi tumeamua kuwajengea
waandishi katika maeneo hayo’’, alisema Sungura.
Waziri
wa Habari, Utamaduni,
Sanaa na Michezo, Mhe. Nape Nnauye (kushoto) akipokea bahasha yenye
mafanikio ya Tanzania Media Foundation ambayo yamefanywa nchini katika
kuwajengea uwezo Waandishi wa habari toka kwa Mkurugenzi wa Tanzania
Media Foundation, Bw. Ernest Sungura 12 Julai, 2016 jjijjini Dar es
Salaam.
Waziri
wa Habari, Utamaduni,
Sanaa na Michezo, Mhe. Nape Nnauye (kulia) akipokea zawadi ya bango la
picha zilizopigwa na baadhi ya Waandishi wa Habari waliowahi kujengewa
uwezo na Tanzania Media Foundation 12 Julai, 2016 jijini Dar es Salaam.picha zote na maelezo
0 comments:
Post a Comment