TTCL yahakikisha huduma bora kwa mashirika na taasisi yatakayohamia Dodoma
Na Georgia Misama –
MAELEZO
Kampuni ya Simu Tanzania
(TTCL) imejipanga kutoa huduma bora kwa mashirika na taasisi zinazotarajia kuhamia Mjini Dodoma.
Hayo yamesemwa na Meneja
Uhusiano TTCL Bw. Nicodemus Thom Mushi
leo Jijini Dar es Salaam alipokuwa akiongea na waandishi wa habari juu ya
mpango wa miaka mitatu wa mageuzi ya kibiashara wa Kampuni hiyo.
Mushi ameeleza kuwa,
katika mpango huo TTCL imejipanga vyema kufanikisha azma ya Serikali ya kuhamia
mjini Dodoma kwa kutoa huduma bora kwani tayari kampuni hiyo ina rasilimali
watu, vifaa na wataalamu wa kutosha katika kutoa huduma za Mawasiliano.
“Nitumie fursa hii
kuwaomba taasisi zote za Umma zinazohamia Dodoma na Taasisi zote kwa ujumla
kutumia huduma za TTCL ambazo zote zimethibitika kuwa ni huduma bora na za
uhakika na zenye gharama nafuu,” amefafanua Mushi.
Aidha, kampuni hiyo
imeboresha njia ya kusikiliza wateja ambapo hivi sasa malalamiko ya wateja
hushughulikiwa ndani ya masaa matatu toka mteja anapotoa taarifa katika kituo
cha huduma kwa mteja.
Akiongelea juu ya
maboresho, Mushi amesema kuwa, kampuni hiyo imeleta huduma mpya ya 4G LET ambayo
inapelekea intaneti yenye kasi zaidi, vile vile imeboresha miundo mbinu ya
mitandao ya simu na data na kuondoa mitambo chakavu.
Sambamba na hayo Mushi
amewahakikishia wateja kuwa TTCL ni kampuni pekee ambayo ni suluhisho la huduma
bora na ya uhakika wakati wote na mahali popote iwe ni nyumbani, sehemu ya kazi
na hata kwenye vyombo vya usafiri kutoka sehemu moja kwenda nyingine.
0 comments:
Post a Comment