Tuesday, August 16, 2016

Pangani yapata Kivuko kipya


Watanzania Milioni 23 kupata namba ya utambulisho wa vitambulisho vya uraia ifikapo Desemba 31, 2016.

Na: Lilian Lundo - MAELEZO
15/08/2016

Mamlaka ya Vitambulisho vya Taifa (NIDA) imeeleza kuwa ifikapo Desemba 31 mwaka huu jumla ya watanzania milioni 23 watakuwa na namba za utambulisho wa vitambulisho vya Uraia.

Kaimu Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano wa Mamlaka hiyo Bi. Rose Mdami amesema kuwa hatua hiyo ni utekelezaji wa agizo Rais, Dkt. John Pombe Magufuli la kuitaka Mamlaka hiyo kuweka saini ya mwombaji na mtoaji wa vitambulisho hivyo.

“Tumeanza kutekeleza agizo la Mhe. Rais tangu mwezi Juni mwaka huu, hii inamaanisha kwamba vitambulisho vyote tulivyochapisha kuanzia mwezi Juni mpaka leo vina saini ya muombaji, saini ya mtoaji na tarehe ya kuzaliwa muombaji” amefafanua Mdami.

Ameeleza kuwa kazi ya ugawaji wa vitambulisho hivyo inasubiri kuzinduliwa na Mhe. Rais Dkt. John Pombe Magufuli atakayekabidhiwa  kitambulisho cha uraia namba moja na baadaye vitambulisho hivyo kugawiwa kwa wananchi  wengine. 

Mdami amesema ifikapo Desemba 31 mwaka huu NIDA itakuwa imetoa namba za utambulisho wa vitambulisho hivyo  kwa watanzania milioni 23 kwa kutumia taarifa za Tume ya Uchaguzi (NEC) zilizo katika vitambulisho vya kupigia kura na kuzihamishia katika kanzi data ya NIDA.

Amefafanua  kuwa ili mwananchi aweze kupata kitambulisho cha uraia atalazimika kufika katika ofisi za NIDA akiwa na vielelezo vinavyoonyesha mwaka wake wa kuzaliwa pamoja udhibitisho wa uraia wake hii ni kutokana na NEC kutokuwa na viambatanisho hivyo.

Amebainisha kuwa mwananchi mwenye namba ya utambulisho anaweza kupata huduma zote zinazohitaji namba ya kitambulisho cha Uraia kutokana na namba hiyo kutobadirika na kuendelea kutumika hata baada ya kitambulisho kuchapishwa.

Amesema mpaka sasa watanzania milioni 2.7 wamekwisha patiwa vitambulisho  hivyo na milioni 6.5 wamesajiriwa kwa ajili ya kupata vitambulisho hivyo. 

Aidha, Vitambulisho hivyo vya zamani vitaendelea kutumika mpaka utakapotangazwa utaratibu wa kuvibadirisha kwa ajili ya kupata vitambulisho vipya.

Pia ametoa ufafanuzi juu ya malalamiko ya baadhi ya watu wanaodai kwamba wa kumekuwa na mlolongo mrefu wa kupata vitambulisho hivyo kwa kueleza kuwa NIDA haina namna ya kufupisha mlolongo huo kwani kufanya hivyo ni sawa na kuuza uraia wa Tanzania.

 Amesisitiza kuwa ni lazima NIDA ijiridhishe juu ya uhalali na sifa za muombaji ni kuwa ni Mtanzania kwa kuambatanisha vielelezo vinavyohitajika.

MWISHO







Share this article :

0 comments:

Post a Comment

 
MZUKA BLOG © Copyright 2014. All Rights Reserved.

Powered by MATERU FROM IBS.
imagem-logoRudi Juu