Mkurugenzi Mkuu wa Ofisi ya Taifa ya Takwimu (NBS) Dkt. Albina
Chuwa akitoa taarifa ya Pato la Taifa Robo ya Pili (Aprili – Juni) ya Mwaka
2016 kwa waandishi wa habari leoSeptemba 29, 2016, jijini Dar es Salaam.
Kushoto kwake ni Kaimu Mkurugenzi wa Takwimu za Uchumi wa ofisi hiyo Bi. Joy
Sawe. Taarifa hiyo imeonyesha kuwa Pato la Taifa limekua kwa kasi ya asilimia
7.9 katika kipindi cha mwezi Aprili hadi Juni 2016 ikilinganishwa na kasi ya
asilimia 5.8 katika kipindi kama hicho mwaka 2015.
Mkurugenzi Mkuu wa Ofisi ya Taifa ya Takwimu (NBS) Dkt. Albina
Chuwa akitoa taarifa ya Pato la Taifa Robo ya Pili (Aprili – Juni) ya Mwaka
2016 kwa waandishi wa habari leo jijini Dar es Salaam. Kulia kwake ni Meneja wa
Takwimu za Pato la Taifa wa Ofisi hiyo Daniel Masolwa. Taarifa hiyo imeonyesha
kuwa Pato la Taifa limekua kwa kasi ya asilimia 7.9 katika kipindi cha mwezi
Aprili hadi Juni 2016 ikilinganishwa na kasi ya asilimia 5.8 katika kipindi
kama hicho mwaka 2015.
(PICHA
NA EMMANUEL GHULA)
NA VERONICA KAZIMOTO
PATO
la Taifa limekua kwa jumla ya thamani ya Shilingi trilioni 11.7 katika kipindi
cha robo ya pili ya mwaka 2016 ikilinganishwa na Shilingi trilioni 10.9 katika
kipindi kama hicho cha mwaka 2015.
Akizungumza
na waandishi wa habari leo jijini Dar es Salaam, Mkurugenzi mkuu wa Ofisi ya
Taifa ya Takwimu (NBS) Dkt. Albina Chuwa amesema ukuaji wa pato la Taifa
umetokana na shughuli za kiuchumi ikiwemo kilimo, mifugo, misitu na uvuvi
ambapo shughuli hizo zimekuwa kwa asilimia 3.2 ikilinganishwa
na ukuaji wa asilimia 1.9 katika kipindi kama hicho mwaka 2015.
Kwa
upande wa shughuli za uchumi za viwanda na ujenzi, Dkt. Chuwa alisema kumekua na
ongezeko la asilimia 20.5 katika kipindi hicho ukilinganisha na ukuaji wa
asilimia 11.2 mwaka 2015 katika shughuli za uchimbaji madini, mawe na kokoto.
Aidha
shughuli za uzalishaji bidhaa na viwanda zimeongeza kwa asilimia 9.1 katika
kipindi cha robo ya pili ya mwaka 2016 ukilinganisha na kasi ya asilimia 5.2 ya
mwaka 2015.
Shughuli
za uchukuzi na uhifadhi, Dkt. Chuwa amesema kuwa shughuli hizo zimekua kwa
kiwango cha asilimia 30.6 zikisababishwa na usafirishaji wa abiria
kwa njia ya reli na barabara ikiwa ni pamoja na usafiri wa UDART.
Vilevile,
shughuli za fedha na bima zimeongezeka kwa kasi ya asilimia 12.5 ikilinganishwa
na asilimia 10.0 iliyopatikana katika kipindi kama hicho mwaka 2015.
Dkt.
Chuwa amefafanua kuwa huduma za elimu zimekua kwa kasi ya asilimia
8.0 katika robo hiyo ya mwaka ikilinganishwa na aslimia 7.4 ya kipindi kama
hicho kwa mwaka 2015 ambapo ukuaji wa shughuli hii imetokana na ongezeko la
wanafunzi waliodahiliwa mwaka 2016.
Kwa upande wa Nchi za Afrika Mashariki ambazo zimeshachambua na
kutoa Pato la Taifa katika kipindi kinachoishia Juni 2016 ni Rwanda ambapo Pato
halisi la Nchi ya Rwanda katika kipindi cha Aprili – Juni 2016 limeendelea
kukua kwa asilimia 5.4 ikilinganisha na asilimia 7.2 ya miezi kama hiyo mwaka
2015.
Takwimu za Pato la Taifa kwa robo mwaka hupimwa kwa kutumia thamani
ya bidhaa na huduma zilizozalishwa nchini katika vipindi vya miezi mitatu
mitatu ambavyo ni Januari – Machi, Aprili – Juni, Julai – Septemba na Oktoba –
Desemba ambapo hujumuisha shughuli zote za kiuchumi, na hutumika katika
kutathmini, kupanga mipango na kutayarisha sera za kiuchumi.
0 comments:
Post a Comment