Mwenyekiti
wa Kamati ya Kitaifa ya Kupambana na Biashara Haramu ya Usafirishaji Binadamu, Vicent
Magere akizungumza na Wajumbe wa Kamati hiyo (hawapo pichani) kabla ya
kumkaribisha Mgeni Rasmi, Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Ndani ya
Nchi, Balozi Simba Yahya (katikati) kufungua mkutano wa kamati hiyo wenye lengo
la kujadili pamoja na kuweka mkakati wa kukabiliana na biashara haramu ya
usafirishaji wa binadamu nchini. Kushoto ni Katibu wa Sekretarieti ya Kitaifa
ya Kuzuia na Kupambana na Biashara hiyo kutoka Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi.
(PICHA NA WIZARA YA MAMBO YA NDANI YA
NCHI).
NA
FELIX MWAGARA, MOHA
NAIBU
Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi, Balozi Simba Yahya amewataka
wajumbe wa Kamati ya Kupambana na Biashara Haramu ya Usafirishaji Binadamu
kuweka mikakati imara ya kupambana na wahalifu wa biashara hiyo nchini.
Akizungumza
kabla ya kufungua mkutano wa wajumbe hao wenye lengo la kujadili na kutengeneza
mkakati wa kukabiliana na biashara hiyo, Balozi Simba alisema biashara hiyo
imekuwa ikiongezeka duniani na wahalifu wakipata faida ya mabilioni ya fedha
kutokana na wahanga, wengi wao wakiwa ni watoto, ambao huporwa utu na uhuru
wao.
“Inawezekana
wengi wetu hatujakutana na aina hii ya uhalifu, lakini unatokea kila siku
duniani kote, na nchi yetu ni mojawapo kati ya nchi zinazoathirika na tatizo la
biashara hii haramu,” alisema Balozi Simba na kufafanua;
“Tanzania
ni chanzo, njia ya kupitia na pia hupokea wahanga wa biashara hii haramu.
Wahanga hawa husafirishwa kutoka maeneo ya vijijini kwenda mijini hapa nchini,
wengine husafirishwa kwenda Ulaya, Marekani, Asia na nchi za Kiarabu kama vile
Oman na Dubai.”
Alisema
watu hao hudanganywa kwa ahadi za kupata ajira nzuri au nafasi za elimu, lakini
mwisho wake huishia kunyonywa, kuwa watumwa wa ndani na kufanyishwa kazi kwa
nguvu.
Hata
hivyo, Simba alisema katika hatua ya kupambana na biashara hii haramu, mwaka
2008 ilitunga sheria ya kudhibiti biashara hiyo hapa nchini, na mwaka 2015
walikamilisha kazi ya kuandaa Kanuni za kutekeleza sheria hii. Aliongeza kuwa,
sheria hii ndiyo ilipelekea kuundwa kwa Kamati na Sekretariet ya kupambana na
biashara hiyo haramu ya usafirishaji binadamu.
“Na
leo Kamati na Sekretarieti mnakutana hapa kwa lengo hilo la msingi, kwamba
mnafanya tathmini ya utendaji wenu tangu mwaka 2012 hadi sasa ili kubaini wapi
mlifanya vizuri na wapi hamkupata mafanikio mliotarajia. Tathmini hii
itawawezesha kuweka mikakati thabiti ya kuzuia na kupambana na tatizo hili hapa
nchini,” alisema Balozi Simba.
Simba
alisema anajua wana mafanikio mengi ambayo Kamati hiyo wameyapata katika
utendaji wao tangu kuanzishwa ikiwemo baadhi yake ni pamoja na kuandaa Kanuni
za sheria ya kupambana na biashara haramu ya usafirishaji binadamu, kuandaa
Mpango Kazi wa Kitaifa wa kupambana na biashara hiyo na kuimarika ushirikiano
wa kiutendaji baina yao na idara zingine za serikali, pamoja na Mashirikia
yasio ya kiserikali na ya Kimataifa mfano Shirika la Kimataifa linaloshughulikia
Wahamaji (IOM).
Kwa
upande wake Mwenyekiti wa Kamati ya Kitaifa ya Kupambana na Biashara Haramu ya
Usafirishaji Binadamu, Vicent Magere, alisema kikao hicho kinawahusisha Wajumbe
wa Kamati na Sekretarieti kutoka Bara na Visiwani ambapo wanakutana kwa
mujibu wa sheria ambapo wanapaswa kukutana mara tatu au nne kwa mwaka.
“Lengo
la kukutana ni kufanya tathmini ya utendaji ili kubaini ni wapi tulifanya
vizuri na wapi hatukufanya vizuri. Kikao hiki pia kinatupatia fursa ya kupanga
mikakati ya utendaji ili hatimaye tuweze kuboresha zaidi utendaji wetu,”
alisema Magere.
Naibu Katibu wa Sekretarieti ya Kitaifa ya
Kuzuia na Kupambana na Biashara Haramu ya Binadamu, John Makuri akizungumza
katika kikao hicho.
Katibu wa Sekretarieti ya Kitaifa ya Kuzuia na
Kupambana na Biashara Haramu ya Binadamu kutoka Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi,
Separatus Fella, akiwasilisha mada juu ya Biashara Haramu ya Usafirishaji Binadamu
na juhudi zilizofanywa na serikali hadi kufikia sasa
Picha ya pamoja
0 comments:
Post a Comment