Friday, October 28, 2016

MSEMAJI WA SERIKALI: MFUKO WA MAFUNZO KUWANUFAISHA WANAHABARI NCHINI.

Na Jovina Bujulu
MAELEZO
Dar es Salaam
27.10.2016

WANATASNIA ya habari nchini wametakiwa kuunga mkono uanzishwaji  sheria ya huduma za habari nchini kwa kuwa muswada uliopo umekusudia kutoa mafunzo yanawasaidia kuwaongezea weledi katika utendaji wao wa kazi.

Hayo yamesemwa na Mkurugenzi wa Habari, Hassan Abbas wakati wa ziara yake ya kutembelea vyombo vya habari leo Jijini Dar es Salaam, ambapo alitoa ufafanuzi kuhusu maudhui yaliyopo katika muswada wa sheria hiyo.

 Aliongeza kuwa mafunzo hayo yatatolewa ndani na nje ya nchi na hivyo kuwasaidia waandishi wa habari wa Tanzania kubadilishana uwezo na ujuzi na  wenzao kutoka nchi mbalimbali duniani.

Mafunzo hayo yatakuhusisha mafunzo ya muda mrefu na mfupi, warsha, makongamano na semina.

Abbas alisema kuwa mfuko huo utakuza programu za uendelezaji wa maudhui ya ndani na nje ya nchi na kuchangia utafiti na maendeleo katika nyanja za habari na mawasiliano ya umma.

Kwa mujibu wa Abbas fedha za mfuko huo zitaidhinishwa na Bunge, misaada na  michango mbalimbali ya hiari kutoka vyombo vya habari.

Aidha Abbas alisema waandishi wa habari kupitia mfuko huo watajengewa uwezo kwenye nyanja mbalimbali ikiwemo kilimo, afya, uchumi, elimu na kadhalika ili kuwawezesha kuripoti na kuandika habari hizo kwa weledi zaidi.
Share this article :

0 comments:

Post a Comment

 
MZUKA BLOG © Copyright 2014. All Rights Reserved.

Powered by MATERU FROM IBS.
imagem-logoRudi Juu