Na. Judith
Mhina na Lilian Lundo - MAELEZO
Serikali kupitia Mradi wa Mpango wa
Kuboresha Elimu – EQUIP (Education Quality Improvement Programme) imeendelea
kuboresha mfumo wa Elimu hapa nchini katika nyanja ya mitaala kwa wanafunzi wa
darasa la kwanza mpaka la tatu, uongozi bora katika shule za msingi pamoja na
mifumo ya utoaji taarifa na takwimu sahihi.
Mratibu wa mradi huo hapa nchini Bw
Johan Bentinck, amesema hayo leo jijini, Dar es Salaam alipokuwa akitoa maelezo
ya utekelezaji wa mradi huo na namna ambavyo umefanikiwa katika
kuboresha Elimu kwa wanafunzi wa shule za msingi katika mikoa saba
hapa nchini.
Mradi huo umetoa fursa kwa walimu
kupata mafunzo ya namna ya ufundishaji bora utakaomuwezesha mwanafunzi wa
darasa la kwanza hadi la tatu kujua kusoma, kuandika na kuhesabu ndani ya muda
mfupi na kwa ufasaha.
Aidha kupitia mradi huo ufundishaji
darasa la Kwanza mpaka la Nne umeboreshwa ambapo mwanafunzi anaweza kuunganisha
maneno kwa kutumia sauti. Vile vile kumekuwepo na njia nyingine za kufundisha
kupitia nyimbo na michezo mbalimbali kwa wanafunzi wa madarasa ya awali.
Pia mradi umewezesha kuanzishwa kwa
madarasa ya awali ambayo hayakuwepo katika shule za msingi zilizoko vijijini.
Wanafunzi wa madarasa hayo wamekuwa wakifundishwa na walimu wa kujitolea kwa
muda wa wiki 12 na baada ya hapo hujiunga na darasa la Kwanza.
Aidha mradi huo umeleta mafanikio
makubwa katika sekta ya Elimu hapa nchini ambapo kasi ya ya kutamka maandiko
kwa mwanafunzi wa darasa la Kwanza mpaka la Tatu ilikuwa 21.3 mwaka 2014 na
sasa ni 30.0
“Mradi huo kwa sasa unahusisha mikoa
ya Dodoma, Kigoma, Shinyanga, Simiyu, Tabora, Mara na Lindi huku mikoa mingine
miwili ya Katavi na Singida inategemea kuongezwa mwaka 2017,”
alifafanua Bentinck.
Mwisho
0 comments:
Post a Comment