Na
Beatrice Lyimo-MAELEZO-
DAR ES SALAAM
10/10/2016
SERIKALI imesema imejipanga
kuhakikisha kuwa idadi kubwa ya wananchi waishio vijijini na mijini hapa nchini wananufaika na huduma
ya upatikanaji wa maji safi na salama ili kuwaondolea kero ya uhaba wa maji watanzania ifikapo mwaka 2020.
Kauli hiyo imetolewa
leo jijini Dar es Salaam na Waziri wa Maji na Umwagiliaji Mhandisi Gerson
Lwenge wakati wa uzinduzi wa Bodi ya wadhamini ya Mfuko wa Maji.
Amesema kuwa Serikali
ya Awamu ya Tano imejipanga kuongeza huduma ya upatikanaji wa maji vijijini kutoka
asilimia 72 hadi asilimia 85 na mijini kutoka asilimia 86 hadi asilimia 95
ifikapo mwaka 2020.
Waziri Lwenge amesema
ili kufikia lengo hilo Serikali itahakikisha inafanyakazi kwa juhudi na weledi
na maarifa ili kuondokana na kero hizo.
“Katika kufikia
malengo ya Serikali kuwa ifikapo mwaka 2020 huduma ya maji inawafikia wananchi
waishio vijijini kwa asilimia 85 kutoka asilimia 72 ya sasa na mijini kwa
asilimia 95 kutoka aslimia 86 ya sasa,” alifafanua waziri Lwenge.
Katika kufanikisha
hilo Waziri Lwenge ameiagiza Bodi hiyo kuwa wabunifu, waadilifu na wachapakazi
ili kuleta mabadiliko ambayo yataiwezesha nchi kuwa nchi ya Uchumi wa kati na ya
Viwanda hasa katika Sekta ya Maji.
Kwa upande wa Katibu
Mkuu wa Wizara hiyo Mhandisi Mbogo Futakamba alisema kuwa matumaini ya Serikali
katika kuimarisha hali ya huduma ya maji vijijini na mjini ni kuona mfuko huo unasimamia
ili kutoa matunda yaliyokusudia.
Aidha, Mhandisi
Futakamba alisema kuwa Bodi ya Wadhamini imekasimiwa jukumu la kusimamia na
kulinda maslahi ya Taifa katika kuhakikisha Sekretarieti ya Mfuko inatekeleza
majukumu kwa mujibu wa Sheria, Kanunu na Taratibu zilizopo.
0 comments:
Post a Comment