Monday, November 7, 2016

BODI YA PAMBA KUHAMIA MWANZA

Na Jacquiline Mrisho – MAELEZO, Dodoma

Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi imejipanga kuhamishia Bodi ya Pamba katika Mkoa wa Mwanza kabla ya Novemba 10 mwaka huu ili kuhakikisha wakulima wa pamba waliopo katika mkoa huo wanapata huduma zilizo bora kwa ukaribu na haraka.

Hayo yamesemwa leo mjini Dodoma na Naibu Waziri wa Wizara hiyo, Mhe.  William Ole Nasha alipokuwa akijibu swali la Mbunge wa Bukombe Mhe. Doto Biteko lililohoji juu ya hatua ya Serikali kwa wakulima walioathirika na pembejeo zilizotolewa ambazo hazikuwa na ubora pamoja na kuhamishia Bodi ya Pamba katika mkoa huo.

”ili kuwafikia kirahisi wakulima wa pamba waliopo mkoani Mwanza, Wizara imeamua kuhamishia Bodi hiyo katika mkoa huo na kwa taarifa zilizopo Bodi hiyo inatakiwa kuhama haraka iwezekanavyo kabla ya Novemba 10 mwaka huu”, alisema Mhe.Ole Nasha.

Kwa upande wa matatizo ya pembejeo, Mhe. Ole Nasha amesema kuwa Serikali tayari ina taarifa kuhusu tatizo lililowapata wakulima wa pamba katika maeneo mbalimbali kwa kusambaziwa viuatilifu pamoja na mbegu ambazo hazikuwa na ubora unaotakiwa hivyo kuathiri wakulima nchini.

“Serikali iliiagiza Tropical Pesticides Research Institute (TPRI) kufanya uchunguzi wa malalamiko ya wakulima ambao ulibaini kuwa viuatilifu hivyo vilikuwa na utendaji hafifu hivyo Serikali itaanza kuzalisha mbegu bora za pamba za UK08 ili kuhakikisha tatizo hili halijirudii tena”, alisema Mhe. Ole Nasha.

Naibu Waziri huyo amefafanua kuwa kufuatia changamoto hizo za uotaji wa mbegu, Serikali iliamua kufanya majaribio ya utoaji wa mbegu ambazo zilikuwa zikisambazwa hapo awali bila kujua ufanisi katika uotaji wake.

Amethibitisha kuwa, matokeo ya jaribio hilo yamewezesha kutoa maelekezo kuhusu aina za mbegu za pamba zenye sifa za msingi ambazo zitasambazwa kwa wakulima katika msimu wa kilimo wa mwaka 2016/2017.

MWISHO.
Share this article :

0 comments:

Post a Comment

 
MZUKA BLOG © Copyright 2014. All Rights Reserved.

Powered by MATERU FROM IBS.
imagem-logoRudi Juu