Saturday, December 10, 2016


MAKAMU WA RAIS WA JICA ATEMBELEA KITUO CHA KUPOZA NA KUSAMBAZA UMEME CHA ILALA-MCHIKICHINI JIJINI DAR ES SALAAM
 Mkurugenzi Mtendaji wa Tanesco, Mhandisi Felchesmi Mramba, (kushoto),  akimwelezea jambo Makamu wa Rais wa Shirika la  Serikali ya Japan, linaloshughulikia uratibu wa misada ya maendeleo ya kimataifa, (JICA), Suzuki Noriko,  kuhusu hatua iliyofikiwa na TANESCO katika uboreshaji wa miundombinu ya kupoza na kusambaza umeme alipotembelea kituo cha kupoza na kusambaza umeme cha Ilala-Mchikichini jijini Dar es Salaam, ambapo JICA inashirikana na serikali katika kukiboresha kituo hicho.
Jengo jipya la kituo cha kupoza na kusambaza umeme cha Ilala-Mchikichini jijini Dar es Salaam, ambacho JICA imechangia ujenzi wake.
NA K-VIS BLOG/KHALFAN SAID
Makamu wa Rais wa Shirika la Serikali ya Japan linaloratibu Misada ya Maendeleo laKimataifa (JICA), Bw. Suzuki Noriko ametembelea kituo kipya cha kupoza na kusambaza umeme cha Ilala-Mchikichini kinachoendeshwa na Shirika la Umeme nchini Tanesco.
Ziara hiyo aliifanya Desemba 9, 2016 ambapo Mkurugenzi Mtendaji wa TANESCO Mhandisi Felchesmi Mramba, alimtembeza kujionea hatua mbalimbali zilizofikiwa katika uboreshaji miundombinu ya TANESCO ikiwemo jingo na mitambo.
Ziara hiyo inakuja mwezi mmoja tu baada ya Waziri Mkuu wa Tanzania, Mh. Kassim Majaliwa, kuzindua kituo cha udhibiti na usimamizi wa mifumo ya usambazaji umeme katika jiji la Dar  es salaam kilichoko Mikocheni jijini Dar es Salaam ambapo kituo hicho cha Ilala, ni sehemu ya mradi wa uboreshaji miundombinu ya umeme kwenye jiji hilo.
JICA na mashirika mengine ya kimataifa yanafadhili mradi huo wa uboreshaji umeme jijini ambapo lengo ni kuwapatia wakazi wa jiji umeme ulio bora na wa uhakika zaidi, ambapo utekelezaji wa mradi huu umehusisha ujenzi wa kituo cha kupoza nguvu za umeme chenye ukubwa wa 100MVA (2X50MVA), 132/33KV cha City Centre, ujenzi wa mfumo wa njia ya usafirishaji umeme chini ya ardhi (Underground Transmission Line) na kwa kutumia minara (Overhead Line) ya msongo wa wa kilovolti 132 kutoka kituo cha Ilala hadi kituo cha City Centre umbali wa Kilomita 3.4, vile vile ujenzi wa mfumo wa njia ya usafirishaji umeme chini ya ardhi, (Underground Transmission Line) kutoka kituo cha Makumbusho hadi kituo cha City Centre umbali wa kilomita 6.67.

Mafundi wa TANESCO kwa kushirikiana na wataalamu kutoka Japan, wakimalizia kazi ya kufunga mitambo kwenye kituo hicho cha Ilala
Share this article :

0 comments:

Post a Comment

 
MZUKA BLOG © Copyright 2014. All Rights Reserved.

Powered by MATERU FROM IBS.
imagem-logoRudi Juu