NA LILIAN LUNDO -
MAELEZO
CHAMA cha Kutetea Abiria Tanzania (CHAKUA) kimeiomba Serikali
kuongeza nguvu na kuhakikisha matumizi ya tiketi za
elekroniki katika sekta ya usafirishaji nchini yanakuwa ya lazima.
Hayo yamesemwa na Afisa Msimamizi wa Chama hicho
ambaye anasimamia Mkoa wa Dar es Salaam Mark Serra, alipokuwa akisoma taarifa
ya chama hicho kwa waandishi wa habari leo, Jijini Dar es Salaam.
“Chakua imekuwa ikifuatilia kwa karibu mfumo huu na kubaini una
manufaa makubwa sana kwa abiria ambapo watatozwa nauli halali iliyoidhinishwa
na Sumatra ambazo ndizo bei elekezi kwa mujibu wa sheria,” alifafanua Serra.
Aliendele kusema kuwa kwa kutumia tiketi za Kielekroniki
itawalazimu wamiliki wa vyombo vya usafiri kutokupandisha nauli
katika kipindi cha mvua au jua kali, kipindi cha wanafunzi wapotoka
vyuoni au mashuleni pamoja na kipindi cha sikukuu au
mwanzoni mwa mwaka, ambapo mabasi mengi huita vipindi hivyo ni vya kuvuna
abiria.
Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Chama hicho Hassan
Mchanjama amesema kuwa mfumo huo utamnufaisha abiria na kuokoa muda
wa kwenda kwenye vituo vya mabasi kwa ajili ya kukata tiketi badala yake mfumo
huu utamuwezesha abiria kukata tiketi akiwa nyumbani, ofisini au
sehemu yoyote aliyopo kwa kutumia simu yake ya mkononi.
Aliongeza kuwa mfumo huo utarahisisha upatikanaji wa taarifa
muhimu za abiria pindi inapotokea ajali kujua abiria wangapi wamepoteza maisha,
waliopata ulemavu pamoja na waliopoteza mali zao, ambapo kwa
mfumo unaotumika sasa hivi ni vigumu kupata takwimu na taarifa sahihi za
abiria.
Hivyo basi kupitia mfumo huo wa kielekroniki CHAKUA itakuwa
katika nafasi nzuri zaidi ya kutekeleza jukumu lake la kumtetea
abiria pindi anapopata tatizo kwa kuwa itakuwa na taarifa sahihi za abiria.
0 comments:
Post a Comment