Tuesday, January 10, 2017

NEC YAONYA WANAOKIUKA MAADILI

NEC YAONYA WANAOKIUKA MAADILI
NA BEATRICE LYIMO-MAELEZO
10/01/2017
Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) imevionya vyama vya siasa na wagombea wanaoshiriki katika uchaguzi mdogo wa mbunge na madiwani kuheshimu na kuzingatia Maadili ya uchaguzi katika kampeni zinazoendelea.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Makamu Mwenyekiti wa tume hiyo Jaji Mkuu Mstaafu wa Zanzibar Hamid M. Hamid alisema kuwa vyama au wagombea watakaokiuka maadili ya Uchaguzi katika mikutano ya kampeni inayoendelea katika maeneo yenye uchaguzi mdogo watachukuliwa hatua.

Alisisitiza kuwa kwa mujibu wa kipendele cha 5.3 cha maadili ya uchaguzi, chama au mgombea atakayekiuka maadili hayo katika jimbo au kata yenye uchaguzi mdogo atafikishwa katika kamati ya maadili ngazi husika na kuchukuliwa hatua stahiki kwa mujibu wa kipengele cha 5.10 cha maadili ya uchaguzi ya mwaka 2015.

“Katika kampeni zinazoendelea, baadhi ya vyama vya siasa vimeanza kukiuka taratibu za kampeni na maadili na kutumia fursa hiyo vibaya ikiwa ni pamoja na kuwasema viongozi vya kitaifa, kutoa matamko ambayo kihalisia siyo ya kumnadi mgombea wao,” alisema Jaji Mst. Hamid.

 “Hivyo Tume inavitaka vyama na wagombea kuheshimu na kuzingatia maadili ya uchaguzi” alisema Mwakamu Mwenyekiti Huyo.

Aidha, Tume ya Taifa ya Uchaguzi inatoa wito kwa wagombea na vyama vya siasa kufanya kampeni za kistaarabu, amani na utulivu, wote wanahimizwa kuzingatia, Sheria za Uchaguzi, Kanuni na Maadili ya Uchaguzi.

Kwa mujibu wa kipengele cha 2.1(m) cha Maadili ya Uchhaguzi, Vyama vya Siasa, wagombea na wafuasi wao wanatakiwa kufanya kampeni kwa kuzingatia misingi inayolenga kutangaza Sera zao ambayo haijengi chuki, mfarakano na mgawanyiko wa jamii.

Kwa sasa vyama vya siasa na wagombea wanashiriki kwenye kampeni za Uchaguzi Mdogo unaotarajiwa kufanyika Januari 22 mwaka huu katika Jimbo la Dimani Zanzibar na kata 20 za Tanzania Bara.
MWISHO


Share this article :

0 comments:

Post a Comment

 
MZUKA BLOG © Copyright 2014. All Rights Reserved.

Powered by MATERU FROM IBS.
imagem-logoRudi Juu