MAONI/HOJA/MTIZAMO
UJENZI
WA UCHUMI WA VIWANDA KUPITIA SEKTA YA UVUVI INAWEZEKANA.
Na Ismail Ngayonga
MAELEZO
DAR ES SALAAM
07.01.2016
KATIKA kufikia uchumi wa kati
ifikapo mwaka 2025, Serikali imekusudia kuweka mkazo katika ujenzi vya viwanda
ili kuharakisha kasi ya ukuaji wa maendeleo kwa wananchi na taifa kwa ujumla.
Ili kufikia lengo hilo, Serikali
imeanisha sekta kuu za kiuchumi ikiwemo mifugo, uvuvi, kilimo, ardhi, nishati,
maji na kadhalika kuwa vipaumbele vikuu vya kimkakati vilivyojengewa uwezo wa
kutumia rasilimali na malighafi ilizonazo hususani katika kuvutia wawekezaji wa
ndani na nje ya nchi.
Idadi ya viwanda hapa nchini
imeendelea kuongezeka kutoka viwanda 125 Mwaka 1961 hadi kufikia viwanda 54,422
mwaka 2016, Aidha, kati ya hivyo, viwanda vikubwa vinavyoajiri kuanzia watu 100
ni 247, viwanda vya kati vinavyoajiri kati ya watu 50 na 99 ni 170, viwanda
vidogo vinavyoajiri kati ya watu watano na 49 ni 6,907.
Kulingana na takwimu hizo, ni
dhahiri kuwa asilimia 99.15 ya viwanda vyote nchini ni viwanda vidogo sana na
viwanda vidogo, ambavyo hutegemea sekta zisizo rasmi katika kutengeneza ajira
za moja kwa moja kwa wananchi.
Uvuvi ni miongoni wa shughuli kuu
ya kiuchumi kwa wananchi wengi wanaozunguka maeneo ya ukanda wa bahari, mito na
maziwa, ambapo hutumia mazao ya rasilimali za maji kwa ajili ya lishe na
kujiongezea kipato.
Akizungumza hivi karibuni Jijini
Dar es Salaam, Katibu Mkuu wa Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi (Uvuvi), Dkt. Yohana
Budeba anasema Serikali imeanza mchakato wa kuwahamisha wananchi kuwekeza
katika viwanda ili kuongeza thamani ya mazao ya uvuvi nchini.
Dkt. Budeba anasema hadi sasa
jumla jumla ya viwanda vidogo vidogo 48 vya kuchakata samaki, ambapo 36 vipo
katika ukanda wa pwani, 11 ukanda wa ziwa Victoria na 1 ukanda wa ziwa
Tanganyika, ambapo vyote kwa pamoja vimekusudia kuongeza ajira na kuondoa umaskini
kwa Watanzania.
“Mwaka 2015 jumla ya tani 42,000
za samaki ziliuzwa na jumla ya Tsh. Bilioni 1.6 ziliweza kukusanywa, hivyo tunaamini kuwa
ujenzi wa viwanda utaweza kuiwezesha sekta hii kuongeza mchango wake katika
pato la taifa kutoka asilimia 2.4 ya sasa” anasema Budeba.
Dkt. Budeba anasema Serikali
imekusudia kujenga vituo vya kutotolesha samaki ili kuwezesha Tanzania kuwa
kuzalisha tani 50,000 za samaki katika kipindi cha miaka mitano ijayo, ambapo
kwa sasa Serikali ipo katika mazungumzo na Serikali ya Japan kwa ajili ya
kujenga vituo katika mikoa ya Tanga, Morogoro na Rukwa.
Anaongeza kuwa kusudio la ujenzi
wa vituo hivyo ni pamoja na kuanzisha mpango wa uzalishaji wa mbegu bora za
samaki ikiwemo sato na sangara, ambao wamekuwa wakipendwa na wananchi kwa ajili
ya matumizi ya kitoweo ili kuchangia lishe bora.
Kwa mujibu wa Dkt. Budeba anasema
ili kuhakikisha wananchi wanafuga kwa kuzingatia kanuni za ufugaji bora,
Serikali imekusudia kusambaza Wataalamu katika kila Kata nchini hatua
inayolenga kuwajengea uwezo wafugaji kufuga kisasa zaidi.
Akifafanua zaidi Dkt. Budeba
anasema Serikali itaendelea kuongeza idadi ya waatalamu wa uvuvi nchini, ambapo
imepanga kuzalisha na maafisa ugani 5000 kupitia vyuo vya mafunzo ya uvuvi vya
Mbegani- Bagamoyo, Nyegezi-Mwanza na Kigoma.
Aidha Budeba anasema Serikali
inaendelea kuwahamisha wafugaji kujiunga katika vyama vya ushirika wa msingi
vilivyopo katika Halmashauri, kwani kupitia vikundi huweza kutoa mikopo na
ruzuku mbalimbali.
“Mwaka 2015/16 Serikali ilitoa
kiasi cha Tsh. Milioni 440 kwa vikundi 73 vya ushirika wa wafugaji samaki, na
pia ruzuku katika vifaa vya uvuvi na vyakula vya samaki, na mashirika ya
hifadhi ya jamii ikiwemo NSSF nao wameanza utaratibu huu” anasema Budeba.
Akizungumzia kuhusu shirika la
Uvuvi Nchini (TAFICO), Dkt. Budeba anasema Serikali imekusudia kurejesha hadhi
ya shirika hilo, ambapo imepanga kununua meli tano kubwa za kisasa ili
kuliwezesha shirika hilo kufanya shughuli za uvuvi katika maji ya kina kirefu.
Jitihada za
Serikali zinazoendelea kuelekezwa katika kuboresha mazingira ya uwekezaji na
biashara na kuendeleza viwanda vidogo, zitasaidia wananchi walio wengi zaidi
kupata ajira, kuongeza kipato na kupunguza umasikini kupitia uvuvi.
Uchumi wa
viwanda kupitia sekta ya uvuvi utaliweka taifa letu kuwa katika kundi la
mataifa yanayozalisha bidhaa bora na zenye ushindani wa soko la kimataifa
badala ya kuwa chanzo cha malighafi na soko la bidhaa kwa viwanda vya mataifa
mengine.
Ili kufikia
azma hiyo, ushirikiano na mchango wa mtu mmoja mmoja, makundi ya watu, taasisi
za umma na taasisi za binafsi utahitajika, hiyo ni pamoja na kila mmoja wetu
kwa uwezo wake kulenga kuwekeza katika viwanda vyetu na kupenda kununua mazao
ya samaki yanayozalishwa nchini.
0 comments:
Post a Comment