-Ni baadhi ya washiriki wa mafunzo hayo
wakifuatilia kwa makini mada zinazowasilishwa wakiwemo makatibu, wenyeviti , wajumbe wa kamati za
siasa za ngazi za matawi hadi majimbo kwa chama na jumuiya zake, yaliyofanyika
katika Ukumbi wa Mkoa wa Mjini Amani Unguja.(PICHA NA AFISI KUU CCM ZANZIBAR).
NA IS-HAKA OMAR, ZANZIBAR.
WAFUASI wa CCM wameshauriwa
kutowachagua baadhi ya wanachama wenye kashfa na tabia za usaliti kuwa viongozi
wa ngazi mbali mbali zinazowaniwa ndani ya chama na jumuiya zake hicho kupitia
uchaguzi unaoendelea hivi sasa.
Ushauri huo umetolewa na Naibu Katibu Mkuu wa Chama hicho
Zanzibar, Dkt. Abdalla Juma Saadala “
Mabodi” katika mwendelezo wa mafunzo
elekezi ya kuwajengea uwezo watendaji na viongozi wa majimbo ya Mkoa wa
Magharibi Unguja, ili waelewe kwa kina Mabadiliko ya Katiba ya CCM na kanuni
mbali mbali yaliyofanyika hivi karibuni mjini Dodoma.
Dkt. Mabodi alisema chama hicho ili kiendelee kuimarika ni
lazima wanachama wake ambao ni waaminifu wafanye maamuzi magumu ya kuwaweka
kando kwa njia ya Kidemokrasia baadhi ya wanachama wenye dalili na sifa za
usaliti sambamba na kamati za maadili kuanzia ngazi za chini kuwafanyia vikao
vya kikanuni kuwajadili na kuwapatia fursa za kujitetea endapo watakutwa na
makosa wachukuliwe hatua kwa mujibu wa maelekezo ya Katiba na kanuzi za maadili.
Pia Dkt. Mabodi alieleza kwamba lengo la kuchukua maamuzi
hayo sio kuwaonea watu hao bali ni kukisafisha chama ili kibaki na wanachama
waadilifu watakaokilinda na kukipigania katika mazingira yoyote hasa wakati wa
chaguzi za chama na dola pamoja na vipindi mbali mbali vya misukosuko ya
kisiasa nchini.
“ Kama tunahitaji
kufanya matengenezo ndani ya nyumba yetu ni lazima nyufa zilizomo zote
tuzibomoe na kuanza kujenda upya awamu kwa awamu kwa nia ya kupata nyumba imara
na ya kudumu, na uko ndiko tunakoelekea
kwa sasa lazima tupate makada wa kweli wanaotamka dhana ya Mapinduzi daima
pamoja na kuulinda muungano kwa vitendo na sio kauli pekee.”, alisema Dkt.
Mabodi.
Akizungumzia mabadiliko ya Katiba ya CCM yaliyofanyika hivi
karibuni, alisema yamelenga kuongeza ufanisi ndani ya chama hicho kwa kupunguza
idadi za viongozi na vikao vilivyokuwa vikitumia fedha nyingi kwa uendeshaji
wake na kubaki na mambo machache yatakayoongeza ufanisi kwa matumizi mazuri ya
rasilimali za chama na kiutendaji.
Naibu Katibu Mkuu huyo aliwaagiza washiriki wa Mafunzo hayo kuwa mabalozi na
walimu wa kuwaelekeza kwa ufasaha wanachama wa CCM ambao hawakupata fursa hiyo
ili nao wajue lengo la mabadiliko.
Hata hivyo aliupongeza Mkoa huo kwa kazi nzuri walioyofanya
katika Chaguzi za Dola za Octoba 2015 na Machi, 2016 kuwa zilizaa matunda ya
kupatikana kwa Serikali ya Awamu ya Saba chini ya Uongozi wa Dkt. Shein pamoja
na viongozi wengine wakiwemo Madiwani, Wawakilishi na Wabunge licha ya kuwepo
kwa changamoto nyingi za kisiasa.
Aidha aliweka wazi kwamba suala la kuimarisha uchumi wa chama
hicho kupitia miradi ya ndani ya chama kuanzia ngazi za matawi hadi taifac
halina mbadala kwani linagusa moja kwa moja maendeleo na kukuza uchumi wa
Taifa.
Akijibu hoja za baadhi ya washiriki wa mafunzo hayo mwasilishaji
wa mada ya mabadiliko ya Katiba ya chama hicho, Alhaji Rajab Kundiya alieleza kwamba ndani ya
maboresho ya kanuni ya uchaguzi haijamzui mfanyakazi wa umma kutowania nafasi
yoyote ya uongozi ndani ya CCM, isipokuwa wafanyakazi wenyewe wana miongozo na
taratibu zao za kiutumishi katika sehemu zao za kazi.
Sambamba na hayo alisema kupitia marekebisho ya kanuzi za
uchaguzi na maadili zimeweka utaratibu mzuri utakaomaliza tabia za kupanga safu
na rushwa ndani ya chama hivyo kutoa fursa kwa wapiga kura kumchangua kiongozi
anayefaa na mwenye sifa zinazokubalika katika michakato ya kidemokrasia na
kiuongozi.
Naye Mwenyekiti wa CCM
Mkoa wa Magharibi, Nd. Yussuf Mohamed Yussuf
alisema washiriki hao ni wadau wakubwa wa masuala ya chaguzi za chama na
dola hivyo wanatakiwa kutumia mafunzo hayo kuongeza uzalendo, uaminifu na umakini zaidi katika uchaguzi huo.
0 comments:
Post a Comment