Friday, May 5, 2017

Na Beatrice Lyimo-MAELEZO 05/05/2017 Dar Es Salama. WAKALA wa Ufundi na Umeme Tanzania (TEMESA) imeunda kikosi kazi maalumu kitakachohusika na zoezi la ukusanyaji wa madeni ya kiasi cha Tsh Bilioni 10 inazodai TEMESA katika taasisi za Serikali. Hadi kufikia mwezi machi mwaka huu TEMESA imekusanya kiasi cha Tsh milioni 157 inazodai kutoka katika taasisi mbalimbali za Serikali. Hayo yamebainishwa na Mtendaji Mkuu wa TEMESA Dkt. Mussa Mgwatu wakati wa mahojiano ya kipindi maalum cha TUNATEKELEZA kinachoratibiwa na Idara ya Habari- MAELEZO na kurushwa hewani na Kituo cha Televisheni ya Taifa (TBC). Dkt Mgwatu alisema kuwa TEMESA ina jukumu la kutoa huduma za kiuhandisi kwa Taasisi za Umma na watu binafsi ikiwemo uzalishaji na utengenezaji magari pamoja na uboreshaji mitambo na huduma za vivuko na huduma za ushauri na uendeshaji. “TEMESA imekuwa ikiongeza vivuko kulingana na mahitaji ya huduma hivyo ina mpango wa kuongeza kivuko kimoja katika eneo la Kigamboni na kufanya vivuko kuwa vitatu vitakavyofanyakazi saa 24 kwa lengo la kurahisisha huduma ya usafishaji” alifafanua Dkt. Mgwatu. Aidha alisema kuwa katika mwaka wa Fedha 2017/2018 TEMESA imepanga kuboresha zaidi matumizi ya TEHAMA kwa lengo la kurahisisha utendaji kazi ndani ya TEMESA na kuboresha huduma ili kuwavutia taasisi na watu binafsi kupata huduma za taasisi hiyo. Vilevile Dkt. Mgwatu aliongeza kuwa kuanzia mwezi Julai mwaka 2017 TEMESA imepanga kupunguza gharama za tozo za utengenezaji wa magari kwa taasisi za umma na watu binafsi. Mbali na hayo Wakala wa Ufundi na Umeme nchini kwa mwaka 2016/2017 imeweza kutekeleza miradi mbalimbali mikubwa iliyokamilika ndani ya muda uliopangwa ambapo imeshiriki pia katika ujenzi wa Hosteli za wanafunzi katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM). MWISHO
Share this article :

0 comments:

Post a Comment

 
MZUKA BLOG © Copyright 2014. All Rights Reserved.

Powered by MATERU FROM IBS.
imagem-logoRudi Juu