TAARIFA
KWA VYOMBO VYA HABARI
Nitatoa kauli kamili
baada ya kupata nakala ya risala iliyosomwa, hotuba zilizotolewa, ripoti za
matukio tajwa na masuala ya ziada yaliyoibuliwa; katika hatua ya sasa natoa
kauli ya awali kwamba:
MAANDAMANO
NI MATOKEO YA UFISADI, UDHAIFU WA SERIKALI NA KUTOKUTEKELEZWA KWA WAKATI KWA
MAAZIMIO YA BUNGE:
Mkutano na Maandamano
ya wananchi wa Mtwara kutaka majibu toka
kuhusu manufaa ya miradi ya gesi
asili inayotoka katika maeneo yao ni matokeo ya madai ya ufisadi wa
baadhi ya viongozi na udhaifu wa Serikali katika kuushirikisha umma katika
michakato ya maamuzi ya kisera na
kitaasisi kuhusu rasilimali na miradi muhimu ya maendeleo.
Aidha, ni matokeo pia
Bunge kutokuisimamia kikamilifu Serikali kwa niaba ya wananchi kwa mujibu wa
ibara ya 63 ya katiba wakati serikali inapoacha kufafanua masuala yanayohojiwa
na wabunge na inapokwepa kutekeleza maazimio ya Bunge kuhusu sekta ya nishati
ikiwemo sekta ndogo ya gesi asili.
Iwapo Serikali
ingezingatia maoni na mapendekezo yaliyotolewa na Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni
mwezi Julai 2011 na Julai 2012 miradi husika ya maendeleo ya gesi asili
ingetekelezwa kwa wakati na kwa ufanisi bila malalamiko makubwa kutoka kwa
wananchi katika mikoa yote inayohusika na miradi hiyo.
RAIS
AHUTUBIE TAIFA KUHUSU GESI NA KUTUMIA MAMLAKA YAKE
Ili kurekebisha hali
hiyo, nashauri Rais Jakaya Kikwete atumie hotuba yake kwa taifa ya mwishoni
mwezi huu wa Disemba 2012 kueleza kwa umma undani wa miradi husika ya gesi
asili na manufaa yake kwa wananchi wa
maeneo husika na nchi kwa ujumla; hatua ambayo alipaswa kuifanya tarehe 8 Novemba 2012 wakati wa uzinduzi wa mradi
husika.
Aidha,
Rais
atumie mamlaka yake kwa
mujibu wa katiba ibara za 33, 34, 35, 36 kuagiza Waziri wa Nishati na Madini
Prof. Sospter Muhongo, watendaji wengine wa Wizara hiyo na taasisi zake pamoja
na watumishi wa umma mbalimbali wanaofanya kazi kwa niaba ya Rais katika maeneo
ambayo miradi hiyo inatekelezwa kuchukua hatua ya kurekebisha udhaifu
uliojitokeza na kutoa ufafanuzi kwa umma kwa kurejea pia masuala wabunge
tuliyahoji kwa nyakati mbalimbali bungeni mwaka 2011 na 2012.
SERIKALI ITEKELEZE MAAZIMIO YA
BUNGE KUHUSU NISHATI IKIWEMO KUREJESHA DOLA MILIONI 20.1 NA KUSHUGHULIKIA MADAI
YA UFISADI
Kabla ya kufafanua kuhusu miradi iliyoanza hivi sasa, Rais au viongozi na
watumishi wengine wa umma watakaozungumza kwa niaba yake waeleze mapato na
manufaa ambayo wananchi wa maeneo husika na nchi kwa ujumla imepata kutoka gesi
ilipoanza kuvunwa katika mikoa ya Kusini mwaka 2004 na hatua ambazo Serikali
imechukua mpaka dhidi ya madai ya ufisadi wa baadhi ya viongozi katika mapato
ya rasilimali hizo muhimu za taifa.
Serikali ieleze
imefikia wapi katika kurejesha kiasi cha dola milioni 20.1 (zaidi ya Bilioni
30) zilizopunjwa kifisadi katika mauzo
ya gesi asili huku miradi ya maendeleo katika maeneo ambayo gesi hiyo imetoka
kama Songosongo na maeneo mengine nchini ikiwa na upungufu wa fedha.
Ikumbukwe kwamba kwa
niaba ya Kambi Rasmi ya Upinzani nilieleza bungeni tarehe 15 Julai 2011 kuhusu
tuhuma za ufisadi na ukiukwaji wa mikataba katika sekta ndogo ya gesi inaoihusu
pia Kampuni ya Pan African Energy Tanzania (PAT) na kutaka kuundwa kwa kamati
teule ya bunge kuchunguza suala hilo.
Badala yake Kamati ya
Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini iliunda kamati ndogo ya iliyofanya
uchunguzi uchunguzi wa masuala husika na taarifa kuwasilishwa bungeni mwaka
2011; hata hivyo mpaka sasa maamizio ya bunge kufuatia taarifa hiyo
hayajatekelezwa kwa ukamilifu.
WAZIRI
MUHONGO ATOE KWA UMMA MATOKEO YA UCHUNGUZI WA MIKATABA YA UTAFUTAJI WA MAFUTA
NA GESI ASILI
Rais aagize Wizara ya Nishati na Madini iweke wazi ripoti na matokeo ya
timu iliyoundwa na Waziri Muhongo kupitia upya kwa mikataba yote
26 ya utafutaji mafuta na gesi asili ili udhaifu katika mikataba uliobainika
mpaka sasa utumiwe na umma kutoa maoni na mapendekezo ya kuboresha sera,
sheria, taasisi na mfumo mzima wa uingiaji wa mikataba kwa maslahi ya wananchi
wa maeneo husika na taifa kwa ujumla.
NAENDELEA
NA KUSUDIO LA KUTUMIA SHERIA KUPATA MIKATABA YA MKOPO WA DOLA BILIONI 1.225 NA
YA MIRADI YA UJENZI WA MIUNDOMBINU YA GESI MTWARA MPAKA DAR ES SALAAM
Kwa upande wangu hata
baada ya maandamano na mkutano wa wananchi wa Mtwara walioufanya wa tarehe 27
Disemba 2012, nitaendelea kutekeleza kusudio langu nililolieleza tarehe 26
Disemba 2012 la kutumia kifungu cha 10 cha Sheria
ya ya Haki, Kinga na Madaraka ya Bunge kutaka nakala ya mkataba wa mkopo wa masharti kiasi cha Dola za Marekani bilioni 1.225 (shilingi trilioni 1.86) kutoka China.
ya ya Haki, Kinga na Madaraka ya Bunge kutaka nakala ya mkataba wa mkopo wa masharti kiasi cha Dola za Marekani bilioni 1.225 (shilingi trilioni 1.86) kutoka China.
Nitataka pia
nakala za mikataba wa mradi wa miundombinu ya gesi asilia ambayo itahusisha
ujenzi wa mitambo ya kusafishia gesi asilia katika mikoa ya Lindi na Mtwara na
ujenzi wa bomba kuu la kusafirishia gesi asilia la inchi 36 kutoka Mtwara
kupitia Lindi, Pwani hadi Dar es Salaam lenye umbali wa kilometa 532.
Hii ni
kwa sababu mpaka sasa Wizara ya Nishati na Madini haijatekeleza pendekezo
nililowasilisha bungeni tarehe 27 Julai 2012 kwamba kutokana na unyeti wa mradi
huo kwa mustakabali wa nchi na maisha ya wananchi wa sasa na baadaye Serikali
ilipaswa kuwasilisha bungeni na kuweka wazi kwa umma mkataba wa mradi husika.
Aidha,
naitaka Serikali irejee mapendekezo
niliyotoa bungeni na kutoa maelezo kwa umma ya sababu za bomba hilo kujengwa
kutoka Mtwara mpaka Dar es salaam na kueleza kwa uwazi manufaa ya mradi huo na
miradi mingine inayopaswa kutekelezwa katika mikoa ya Kusini kwa maendeleo ya
wananchi husika.
Ikumbukwe
kuwa tarehe 27 Julai 2012 nilieleza bungeni kuwa pamoja na ujenzi wa mitambo miwili ya
kusafishia gesi asili Mnazi Bay na Songo Songo kama sehemu ya mradi huo;
Serikali inapaswa kueleza ni miradi ipi inayoambatana na mradi huo ambayo
imepangwa kuwanufaisha wananchi wa mikoa ya Lindi na Mtwara ikiwemo kuharakisha
utekelezaji wa mradi wa kuzalisha umeme wa MW 300 Mtwara na MW 230 wa Somanga
Fungu (Kilwa).
SPIKA AELEKEZE KAMATI MBADALA YA KUISIMAMIA SERIKALI KWA
NIABA YA BUNGE KUHUSU NISHATI NA MADINI
Kwa
upande mwingine, utekelezaji wa mradi huo unaendelea bila kuwa na Kamati ya
Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini ambayo ingepaswa kuishauri na kuisimamia Serikali hivyo ni muhimu Spika wa
Bunge akachukua hatua kutokana na barua niliyomwandikia mwanzoni mwa mwezi
Oktoba 2012 ambayo mpaka sasa haijajibiwa.
Izingatiwe
kwamba katika barua hiyo nilitoa mwito kwa Spika atumie madaraka na mamlaka yake kutangaza kwa umma kamati
nyingine ya kudumu ya Bunge itayoshughulikia nishati na madini ikiwemo masuala
ya gesi asili kwa sasa kufuatia hali tete na tata kuhusu sekta ndogo ya gesi
asili nchini na kwa kuzingatia umuhimu na unyeti wa sekta hiyo katika uchumi wa
nchi na maisha ya wananchi.
John Mnyika (Mb)
Waziri Kivuli wa Nishati na Madini
28/12/2012
0 comments:
Post a Comment