Sunday, July 14, 2013


MKUTANO TFF WAPITISHA MAREKEBISHO YA KATIBA

Mkutano Mkuu Maalumu wa Shirikisho la Mpira wa Miguu (TFF) uliofanyika leo (Julai 13 mwaka huu) umepitisha marekebisho ya Katiba yake, hivyo mchakato wa uchaguzi unatarajia kuanza wakati wowote.



Wajumbe zaidi ya 100 walihudhuria Mkutano huo uliofanyika ukumbi wa NSSF Waterfron, Dar es Salaam na kufunguliwa na Mkuu wa Mkoa wa Morogoro, Joel Bendera aliyewataka wajumbe kuhakikisha kiwango cha mpira wa miguu nchini kinakuwa.



Mkutano huo uliokuwa chini ya uenyekiti wa Rais wa TFF, Leodegar Tenga umefanya marekebisho ya Katiba kutokana na maelekezo ya Shirikisho la Kimataifa la Mpira wa Miguu (FIFA). James Johnson kutoka Idara ya Wanachama ndiye aliyeiwakilisha FIFA katika mkutano huo.



Aprili mwaka huu FIFA ilisimamisha mchakato wa uchaguzi wa TFF, na kuagiza kwanza yafanyike marekebisho ya Katiba ili kuingiza Kamati ya Maadili, na Kamati ya Rufani ya Maadili ambavyo ndivyo watashughulikia matatizo ya kimaadili kwa familia ya mpira wa miguu nchini.



Mbali ya kamati hizo, mabadiliko hayo pia yametengeneza ngazi mbili za kushughulikia masuala ya kinidhamu ambazo ni; Kamati ya Nidhamu na Kamati ya Rufani ya Nidhamu.



Kamati ya Utendaji ya TFF chini ya Rais Tenga itakutana kesho (Julai 14 mwaka huu) kwa ajili ya kuteua wajumbe watakaounda Kamati hizo ili kuruhusu kuanza mchakato wa uchaguzi ambao FIFA iliusimamisha hadi vitakapoundwa vyombo hivyo.



TAIFA STARS YAPOTEZA MECHI NYUMBANI

Taifa Stars imeshindwa kuutumia vizuri uwanja wa nyumbani baada ya leo (Julai 13 mwaka huu) kufungwa bao 1-0 na Uganda (The Cranes) katika mechi ya kwanza ya mchujo kuwania tiketi ya kucheza Fainali za Wachezaji wa Ligi za Ndani (CHAN) zitakazofanyika mwakani nchini Afrika Kusini.



Denis Iguma ndiye aliyefunga bao hilo pekee kwa Uganda dakika moja baada ya mwamuzi Thierry Nkurunziza kutoka Burundi kupuliza filimbi kuanzisha kipindi cha pili cha mechi hiyo iliyochezwa Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.



Akizungumzia matokeo hayo, Kocha wa Stars, Kim Poulsen amesema mpira wa miguu ni mchezo wa kufunga mabao ambapo timu ilipata nafasi nzuri katika dakika ya kwanza tu lakini ilishindwa kuibadili kuwa bao.



“Uganda walitengeneza nafasi moja tu katika kipindi cha kwanza wakati sisi tulikuwa nazo kadhaa. Kipindi cha pili tuliwapa nafasi wakafunga bao lao. Lakini kwa kifupi kama wao wameweza kufunga hapa (Dar es Salaam), hata sisi tunaweza kufunga Kampala,” amesema Kim akizungumzia nafasi ya timu yake kusonga mbele.



Timu hizo zitarudiana jijini Kampala kati ya Julai 26 na 27 mwaka huu ambapo mshindi ndiye atakayepata tiketi ya kwenda kwenye fainali za tatu za CHAN zitakazofanyika Afrika Kusini. Stars ilicheza fainali za kwanza za CHAN zilizofanyika mwaka 2009 nchini Ivory Coast.



Boniface Wambura

Ofisa Habari

Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF)


Share this article :

0 comments:

Post a Comment

 
MZUKA BLOG © Copyright 2014. All Rights Reserved.

Powered by MATERU FROM IBS.
imagem-logoRudi Juu