Rais wa Jamhuri ya Muungano wa
Tanzania, Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete ameahidi kuwa Serikali yake
imedhamiria na itahahakisha kuwa inalimaliza balaa la watu kumwagiwa tindikali
iwe ni Zanzibar ama Tanzania Visiwani.
Hata hivyo, Rais Kikwete amesema kuwa
katika siku za karibuni Jeshi la Polisi lilifanya operesheni kubwa katika mitaa
ya Zanzibar ambako watu 10 wametiwa mbaroni kwa tuhuma za kushiriki mipango ya
kuandaa na kutekeleza vitendo hivyo.
Rais amemwambia Katibu Mkuu wa Umoja
wa Mataifa (UN) Mheshimiwa Ban Ki Moon kuwa chimbuko la tatizo hilo lina sura
nyingi lakini hakuna shaka kuwa katika kipindi kifupi iwezekanavyo Serikali
itafikisha tatizo hilo mwisho wake.
Rais Kikwete ametoa msimamo huo wa
Serikali kuhusu vitendo ambavyo vimekuwa vinaongezeka vya watu mbali kushambuliwa
kwa kumwagiwa tindikali, tatizo ambalo kimsingi lilitokea kwa mara ya kwanza
Zanzibar wakati kiongozi maarufu wa Kiislamu Sheikh Soroga alipomwagiwa
tindikali akifanya mazoezi ya viungo asubuhi moja kwenye mitaa ya mji wa
Unguja.
Rais Kikwete ametoa msimamo huo wakati
alipokuwa anazungumza na Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa ofisini kwake mjini
New York, Marekani, leo, Ijumaa, Septemba 27, 2013 baada ya kuwa ameulizwa
jambo hilo na Mheshimiwa Ban Ki Moon kuhusu tatizo hilo.
“Ni kweli tumekuwa na vitendo hivyo, zaidi
Visiwani Zanzibar kuliko Bara ambako hata hivyo nako vimekuwepo vitendo hivyo.
Ni jambo la kulaaniwa sana na karibuni Jeshi la Polisi lilifanya operesheni
maalum na msako mkubwa Tanzania Visiwani ambako watu 10 wametiwa mbaroni na
watafikishwa katika vyombo vya sheria.”
Amesisitiza Rais Kikwete: “Wakati
lilipoanza tatizo hilo, tulidhani kuwa alikuwa ni Sheikh Soroga aliyekuwa
anatafutwa peke yake na watu ambao walikuwa hawakubaliani kisiasa na msimamo
wake,lakini mara wakaanza kushambuliwa watu wengine wakiwemo wasichana wawili
wa Uingereza ambao walikuwa wanafanya kazi za kujitolea tu. Tatizo hili ni
lazima likome.”
Imetolewa na:
Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais,
Ikulu,
DAR ES SALAAM.
0 comments:
Post a Comment