Mwenyekiti wa CCM
Taifa, Rais Mstaafu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania awamu ya Nne Dkt.Jakaya
Mrisho Kikwete
akipokea
barua ya uteuzi kutoka kwa Prof. Faustin Kamuzora kwenye ofisi ndogo za
makao makuu ya CCM barabara ya Lumumba jijini Dar es Salaam
Mwenyekiti wa CCM
Taifa, Rais Mstaafu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania awamu ya nne Dkt.Jakaya
Mrisho Kikwete akizungumza na Faustin Kamuzora alipofanya ofisi za CCM Lumumba
NA MWANDISHI MAALUM
KITUO cha Ufundi cha
Kilimo na Maendeleo Vijijini (Technical Centre for Agricultural and Rural
Cooperation, CTA) kilicho chini ya Umoja wa Ulaya (EU) chenye makao makuu mjini
Wageningen, Uholanzi kimemteua Rais Mstaafu Dk. Jakaya Kikwete kuwa
Balozi wa Heshima (Goodwill Ambassador) wa Maendeleo ya Kilimo katika Mabara ya
Afrika, Karibiani na Pacific.
Katika barua iliyokabidhiwa na mjumbe wa Bodi ya CTA, Prof. Faustin
Kamuzora, CTA wameainisha kuwa Dk. Kikwete ambaye pia ni Mwenyekiti wa CCM
Taifa, ameteuliwa kwa kutambua mchango na juhudi zake katika kukiendeleza
kilimo nchini Tanzania na barani Afrika.
Katika wadhifa wake huo mpya, CTA imemuomba Dk. Kikwete aweze
kuiwakilisha katika makongamano ya kimataifa ambapo atazungumzia umuhimu wa
kukiendeleza kilimo kwa ajili ya kutoa fursa ya ajira zenye staha na uhakika
kwa vijana na wanawake katika nchi za barani Afrika, Karibiani na Pasifiki. Pia
ataisaidia CTA katika kuandaa makala na kufanya mahojiano na waandishi wa
habari katika nchi mbalimbali.
Dk. Kikwete amekubali uteuzi huo na kuahidi kushirikiana na CTA katika
kutekeleza mambo ambayo ameombwa kuisaidiana na taasisi hiyo ambayo ni ya
ushirikiano wa Umoja wa Ulaya na Kundi la nchi za Afrika, Karibiani na Pasifiki
wenye makao makuu mjini Brussels, Ubelgiji.
Faustin Kamuzora ambaye pia ni Katibu Mkuu, Mawasiliano ni mjumbe wa Bodi ya CTA
akiwakilisha nchi za ukanda wa Afrika Mashariki kwa miaka mitano tangu 2013
hadi 2018
0 comments:
Post a Comment