Na
Jacquiline Mrisho - MAELEZO
Mamlaka
ya Mapato Tanzania (TRA) imetoa ufafanuzi juu ya utozwaji wa kodi za misaada
inayotolewa na wadhamini kusaidia Sekta ya Maendeleo ya Michezo Nchini.
Ufafanuzi
huo umetolewa leo na Mkurugenzi wa Huduma na Elimu kwa Mlipa Kodi, Richard
Kayombo kutokana na habari iliyochapishwa kwenye baadhi ya vyombo vya habari
kuhusu Serikali kukosa mabilioni ya fedha kwa sababu ya kutokukusanya kodi ya fedha
zinazotolewa na wadhamini kwenda kwa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF).
“Fedha
zinazotolewa kama msaada kutoka kwa wadhamini huwa hazikatwi kodi lakini TRA
hupata mapato yake kutokana na matumizi ya fedha hizo hasa pale wahusika wanapozitumia
katika shughuli za kiuchumi”,alisema Kayombo.
Kayombo
ametaja baadhi ya shughuli za kiuchumi zinazoweza kuwaingizia mapato kutoka
kwenye misaada hiyo kuwa ni; kodi za waajiriwa wakiwemo makocha na wachezaji, makusanyo
ya uwanjani ,kupewa huduma za kitaalam pamoja na majengo ya kupangisha au
kupanga.
Amefafanua
kuwa kama Shirikisho la Mpira wa Miguu Nchini (TFF) linakodisha jengo basi fedha wanazopata
lazima walipe kodi ya asilimia 10 kutoka kwenye fedha hizo na kama wao ndio
wamekodi jengo kwa ajili ya matumizi yao wanatakiwa kutoa kodi ya asilimia 5.
Kwa
upande wa kodi kutoka kwa waajiriwa, Mamlaka hiyo inaendelea kutoa elimu kwa
vilabu vya michezo kuwa michezo ni ajira kama ajira zingine hivyo mishahara yao
inatakiwa kukatwa kodi kulingana na kiasi wanacholipwa.
Zoezi
la kuwatoza kodi makocha na wachezaji limeanza rasmi mwaka huu.
0 comments:
Post a Comment