Na
Raymond Mushumbusi -WHUSM
Waziri
wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo Mhe. Nape Moses Nnauye amewataka
watendaji na watumishi wa Wizara yake kuzingatia maadili na uwajibikaji katika
utekelezaji wa majukumu yao.
Ameyasema
hayo wakati akifungua Baraza la wafanyakazi la Wizara yake na kusisitiza kwa watendaji
kuwasimamia watumishi walio chini yao kuzingatia maadili na uwajibikaji katika
utekelezaji wa majukumu yao katika kutoa huduma kwa wananchi.
Ameongeza
kuwa kuwepo kwa ushirikiano kati ya uongozi na watumishi utasaidia kufanikisha
masuala mbalimbali ya maendeleo ya Wizara, Taasisi zake na watumishi katika
kuleta maendeleo ya Wizara katika kutimiza wajibu wao.
“Nawataka
watumishi wazingatie maadili katika kutekeleza wajibu wao na naamini kwa juhudi
za Serikali ya Awamu ya Tano tutarudisha
maadili ya Utumishi wa Umma na bado taratibu zinaendelea kusimamiwa ipasavyo”asisitiza
Mhe Nnauye.
Mhe.
Nnauye amesisitiza kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt John Pombe
Magufuli ana mpango wa dhati wa kurujesha maadili katika Utumishi wa Umma na
kuhakikisha heshima yake inarudi.
Alieleza
kuwa endapo kuna mtumishi yoyote atakayeshindwa kusimamia suala zima la maadili
anapoteza utumishi wake.
“
Wananchi ndiyo tunaowatumikia na ndiyo wanaotufanya tuwepo hapa tulipo
wanahitaji huduma bora. Kama hatutazingatia suala la maadili ni hakika
hatutaweza kuwatumikia vema” alieleza.
Kwa
upande wake Katibu Mkuu Wizara hiyo , Prof Elisante Ole Gabriel ameahidi
kutekeleza agizo hilo kwa kuhakikisha watumishi
wanazingatia maadili na suala hili linafanyika kwa vitendo zaidi na sio maneno
ili kuendelea kuunga mkono jitihada za Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe.
Dkt John Pombe Magufuli za kurudisha maadili katika Utumishi wa Umma.
“Mhe.
Waziri nakuahidi mimi pamoja na watendaji wenzangu tutalisimamia suala hili na
kulitekeleza kwa vitendo ili turudishe heshima ya utumishi wa Umma kwa kutoa
huduma bora kwa wananchi na kurudisha uaminifu kwa wananchi”alisema Prof
Gabriel.
Kwa
upande wake Mwenyekiti wa TUGHE Tawi la Wizara ya Habari Utamaduni Sanaa na
Michezo Bibi Magreth Mtaka amesema kuwa ni jambo muhimu kwa watumishi
kuzingatia maadili katika utekelezaji wa majukumu yao katiKa eneo la kazi.
“Niwashauri
watumishi wenzangu tuzingatie maadili ya Utumishi wa Umma ili turudishe heshima
ya utumishi wa umma na tutoe huduma iliyo bora kwa wananchi” alisema Bibi
Magreth.
MWISHO.
0 comments:
Post a Comment