Tuesday, January 10, 2017

SERIKALI YA CHINA YAIMWAGIA SIFA TANZANIA KATIKA MIRADI YA UJENZI

Na Ismail Ngayonga
MAELEZO
Zanzibar
10.01.2017

SERIKALI ya China imeisifu Tanzania kwa kuzingatia sera ya uwazi katika ushindanishaji wa zabuni za miradi ya ujenzi, ikilinganishwa na nchi nyingine zilizopo katika ukanda wa  Jumuiya ya Afrika Mashariki.

Hayo yamesemwa leo Mjini hapa na Mwenyekiti wa kampuni ya Kimataifa ya Ujenzi ya CRJE ya nchini China, Bw. Hu Bo wakati  akizungumza na waandishi wa habari  wa Kituo cha Televisheni ya Taifa ya nchi hiyo (CCTV) waliofika nchini kujionea miradi mbalimbali inayotekelezwa na Serikali ya nchi hiyo Tanzania.

Hu Bo alisema Tanzania ni miongoni mwa nchi chache Barani Afrika zinazoongoza kwa kufuata kanuni, sheria na taratibu za zabuni za ujenzi, ambapo Serikali imekuwa ikitoa kipaumbele kwa makampuni ya ukandarasi yanayomilikiwa na wazawa na kukubali maombi yao ya zabuni za ujenzi.

“CRJE tunafanya shughuli zetu katika mataifa mbalimbali ya Afrika Mashariki ikiwemo Kenya, Uganda, Burundi na Rwanda, katika sehemu zote Tanzania imekuwa  nchi bora zaidi kwani pamoja na mazingira salama ya kazi zetu lakini pia wakandarasi wazawa wamekuwa wakipewa nafasi katika miradi ya ujenzi” alisema Hu Bo.

Kwa mujibu wa Hu Bo alisema tangu mwaka 1977 kampuni hiyo imekuwa ikitekeleza miradi mbalimbali ya ujenzi nchini, ambapo mbali  na mazingira bora ya uwekezaji yaliyopo nchini lakini pia kunatokana ushirikiano na uhusiano wa kirafiki uliopo baina ya Serikali ya China na Tanzania.

Aliitaja baadhi ya  miradi ya ujenzi ya Serikali iliyotekelezwa kampuni hiyo nchini ni pamoja na ujenzi wa ukumbi wa Bunge Dodoma, Jengo  la Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais Zanzibar, Jengo la Ofisi ya Wizara ya Katiba na Sheria Zanzibar, Ofisi za Bodi ya Mapato Zanzibar (ZRB).

Aidha Hu Bo alisema kampuni hiyo pia imekamilisha ujenzi wa majengo ya hoteli mbalimbali za kitalii ikiwemo hoteli za kulala wageni za Melia, Tembo, Packyard, Residence, zilizopo Zanzibar pamoja na  Ujenzi wa hoteli ya nyota tano Jijini Mwanza, Hyatt Regency ya Mjini Arusha na Ujenzi wa Daraja la Nyerere, lililopo Kigamboni Jijini Dar es Salaam.

Aliongeza kuwa kampuni hiyo imeendelea kuaminiwa na Serikali na mashirika ya kimataifa kutokana na kuzingatia ubora wa kazi, muda na thamani ya pesa, hivyo aliwataka wakandarasi wa makapuni ya Tanzania kuzingatia vigezo hivyo pindi wanapopewa zabuni za ujenzi wa miradi mbalimbali.

“Kutokana na mafanikio makubwa yaliyofanywa na CRJE, tulishinda tuzo ya kampuni bora ya ukandarasi kutoka nje kwa 2009, 2012 na 2015 katika Tanzania, hii imetupa heshima na kutufanya kuongeza viwango vya ubora katika miradi ya ujenzi tunayoisimamia” alisema Huo Bo.

Alisema Serikali ya China itaendelea kushirikiana na Serikali ya Awamu ya Tano ili kuhakikisha kuwa miradi mbalimbali ya ujenzi inayotekelezwa na Serikali ya China inakamilika kwa wakati na kuzingatia ubora uliowekwa.
MWISHO

Share this article :

0 comments:

Post a Comment

 
MZUKA BLOG © Copyright 2014. All Rights Reserved.

Powered by MATERU FROM IBS.
imagem-logoRudi Juu