Watanzania Tumuunge Mkono Rais Magufuli Kujenga Uchumi Wa Viwanda
Na.
Lilian Lundo - MAELEZO
Katika hotuba yake ya
kwanza Mhe. Rais wa Awamu ya Tano Dkt. John Pombe Magufuli
alipokuwa akifungua Rasmi Bunge la 11 la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania alisema
kwamba Serikali yake itaweka mkazo mkubwa katika ujenzi wa Viwanda.
“Viwanda
tunavyovikusudia ni vile ambavyo sehemu kubwa ya malighafi yake itatoka ndani,
hususani kwenye sekta za kilimo, mifugo, uvuvi, madini na maliasili nyingine,”
alifafanua Rais Magufuli
Viwanda hivyo vitatakiwa kuzalisha bidhaa ambazo zitatumiwa
na watu wengi nchini kama vile nguo, viatu, mafuta ya kupikia ili kuwa na
uhakika wa soko la ndani kabla ya kufikiria soko la nje.
Licha ya Serikali
kuweka mkazo katika uanzishwaji wa viwanda nchini lakini bado watanzania
wamekuwa na fikra potofu juu ya bidhaa zinazotengenezwa ndani ya nchi, wengi
wao wanashusha thamani ya bidhaa hizo na
kuziweka katika kundi la bidhaa zisizo
na ubora huku wakikimbilia bidhaa za nje ya Tanzania.
Waziri wa Fedha na
Mipango Dkt. Philip Mpango alipotembelea maonyesho ya Viwanda yaliyofanyika kuanzia tarehe 07 hadi 11 Desemba 2016 alisema kwamba Tanzania
haitaweza kuwa Tanzania ya Viwanda ikiwa watanzania wenyewe hawathamini bidhaa
zinazotengenezwa ndani ya nchi.
Dkt. Mpango alitoa
mfano wa mashine zinazotengenezwa na SIDO ambazo zimekuwa zikidharaulika kwamba
hazina ubora wakati huo huo mashine hizo zimetengenezwa kwa kuzingatia
mazingira ya nchi yetu na gharama yake ni ya chini ukilinganisha na zile zinazotengenezwa
nje ya nchi.
“Haiwezekani hata
jembe la mkono liagizwe toka nje wakati kuna viwanda ndani ambavyo vinauwezo wa
kutengeneza majembe katika kiwango cha juu.” Alisema Dkt. Mpango.
Ni muda wa watanzania
kubadilika na kuunga mkono Serikali ya Awamu ya Tano kwa kununua bidhaa
zinazotengenezwa ndani ya nchi ili kuipeleka nchi kuwa na uchumi wa viwanda
hatimaye kufikia uchumi wa kati.
Kamwe Tanzania
haitaweza kufikia uchumi wa viwanda ikiwa sisi wenyewe tunakimbilia bidhaa
zinazotoka nje ya Tanzania.
Ifike hatua tuone bidhaa
zetu ni bora zaidi kuliko bidhaa kutoka nje ya nchi. Nchi nyingi zimeendelea
kutokana na kuthamini bidhaa ambazo zimekuwa zikitengenezwa ndani ya nchi.
Mfano ni Nchi ya
Japan, ambayo imekuwa ikifanya vizuri katika uchumi wa viwanda, mafanikio hayo
yametokana na wajapani wenyewe kutokana na imani ambayo wamejiwekea kwamba hakuna
bidhaa inayotengenezwa Dunia yenye ubora zaidi ya bidhaa zinazotengenezwa
nchini kwao.
Kwa kupenda bidhaa
zinazotengenezwa ndani kutaamsha morali kwa uanzishwaji wa viwanda vingi hapa
nchini, kwani watu wengi wamekuwa wakihofia kuanzisha viwanda vidogo vidogo kwa
hofu ya kukosa masoko ya bidhaa zao na wengine wakihofia gharama ya uanzishwaji
wa viwanda.
Ambapo wengi wetu
tumekuwa tukitafsiri kiwanda kama ni kuwa na mashine kubwa, zenye gharama kwa
ajili ya uzalishaji wa bidhaa mbalimbali, na kusahau kuwa kiwanda kinaweza
kuundwa kwa kuwa na cherehani nne tu.
Hivyo basi, kwa kuwa
na cherehani nne peke yake, tayari watu wanne wanakuwa wamepata ajira na
kujikomboa kiuchumi.
Hivyo uchumi huu wa
viwanda ni fursa kubwa kwa vijana katika kutengeneza ajira badala ya kusubiri
ajira kutoka Serikalini au Mashirika Binafsi.
Ambapo Mhe. Rais
katika hotuba yake ya kufungua Bunge la 11 alisema kuwa ifikapo mwaka 2020
idadi ya ajira itokanayo na viwanda ifikie asilimia 40 ya ajira zote
zitakazokuwepo nchini wakati huo.
Mwisho…..
0 comments:
Post a Comment