FIFA kuongeza fedha za Maendeleo na Kujiendesha kwa Shirikisho
Na Anitha Jonas –WHUSM
24/02/2018
Dar es Salaam.
Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) kuendeleza viwanja tisa nchini kufuatia
kuongezeka kwa dau la pesa za Maendeleo na Kujiendesha zinazotolewa na
Shirikisho la Mpira wa Miguu Duniani FIFA kuanzia mwaka 2019 .
Kauli hiyo imetolewa leo jijini Dar es Salaam na Waziri wa Habari Utamaduni Sanaa
na Michezo Dkt.Harrison Mwakyembe alipokuwa akizungumza na vyombo vya habari
kuhusu mambo mbalimbali serikali iliyojadili na Rais wa FIFA Gianni Infantino
alipokuwa nchini kwa mkutano wake hivi karibuni.
‘’Rais wa FIFA alieleza kuongeza mara nne ya kiwango cha pesa za maendeleo na
kujiendesha walizokuwa wanatoa kwa mashirikisho kama TFF mpaka kufikia Dola
Milioni Moja na Laki Mbili na Nusu kwa mwaka na kusema pesa hizo ndiyo zitumike
kuendeleza viwanja vya michezo kwani uwepo wa viwanja ndio unaosaidia kukuza
vipaji vya soka,’’alisema Dkt.Mwakyembe.
Akiendelea kuzungumza katika mkutano huo na waandishi wa habari Waziri
Mwakyembe alisisitiza kuwa Rais huyo wa FIFA ametoa msisitizo wa kutokuwa na
huruma kwa kiongozi yoyote wa shirikisho atakayekuwa na matumizi mabaya ya
pesa pamoja na kufanya udanganyifu kwani yeye yuko mstari wa mbele kupinga
ufisadi katika sekta ya maendeleo ya Soka duniani.
Pamoja na hayo nae Rais wa TFF Bw. Wallace Karia alitoa ufafanuzi wa hali ya
kifedha kwa shirikisho na kueleza kufuatia kuwepo na matatizo katika shirikisho
hilo FIFA ilikuwa imesitisha kuwapatia fedha hizo za maendeleo na kujiendesha
tangu mwaka 2015 lakini baada ya kuingia uongozi mpya ambao FIFA wameridhika
nao na wameshaupa utaratibu wa kufuatilia fedha hizo.
‘’Rais wa FIFA alitueleza kuwa fedha hizo ziko salama nchini Zurich ni kwamba tu
hazikuwa zimeruhusiwa kuingia nchini na kwa sasa tumeshaanza mchakato wa
kufuatilia fedha hizo kwa kuzingatia maelekezo ya FIFA hivyo basi tutakapo pata
fedha hizo Shirikisho litaendeleza baadhi ya miradi ambayo tumekwisha
iandaa,’’alisema Bw. Karia.
Pamoja na hayo rais huyo alitoa wito wa wakazi wa jiji la Tanga waliyovamia eneo
linalotarajia kujengwa Technical Center ya mchezo wa soka basi waondoke mara
moja kabla hawajachukuliwa hatua.
***************MWISHO********************
0 comments:
Post a Comment