Monday, May 14, 2018


JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA
Tanzania Emblem RGBWIZARA YA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO




TAARIFA KWA UMMA KUHUSU MAADHIMISHO YA SIKU YA FAMILIA DUNIANI MEI 15, 2018

Maadhimisho ya Siku ya Familia Duniani ambayo ufanyika kila ifikapo tarehe 15 Mwezi Mei ya kila mwaka, yataadhimishwa katika ngazi ya Mkoa hapa Nchini huku familia za kitanzania bado zikikabiliwa na changamoto ya mila na desturi zenye madhara na ukatili wa kijinsia na watoto ndani ya familia.

Taarifa ya vichocheo vya ukatili nchini  ya mwaka 2015 inaonesha kwamba wanaotekeleza vitendo vya ukatili ni watu wa karibu na familia au wanafamilia wenyewe. Aidha, taarifa ya vitendo vya ukatili vilivyoripotiwa na Jeshi la polisi kwa mwaka 2017 vilikuwa 13,457.

Ili kukabiliana na madhara na changamoto zitokanazo na vitendo hivi vya ukatili katika ngazi ya familia na jamii kwa ujumla Serikali imeandaa kitini cha malezi kwa ajili ya  kutoa elimu malezi na hatimaye kupunguza matukio ya ukatili katika ngazi ya familia.

Juhudi ya kutoa elimu ya malezi katika familia itasaidia wazazi kuwa na mbinu za kuweka mazingira rafiki kwa watoto na ikiwa ni pamoja na kutenga muda wa kutosha kukaa na kujadiliana masuala mbalimbali kwa lengo la kujenga mahusiano yatakayowandaa kudumisha fikra za uzalendo, utu na maadili mema katika kutumia familia zao na Taifa kwa ujumla.  

Hadi sasa mafunzo hayo yametolewa kwa wazazi 3,600, viongozi wa Serikali za vijiji 113, Maafisa Maendeleo ya Jamii na Ustawi wa Jamii Kutoka Halmashauri 76, wanafunzi 10,046, walimu 486, viongozi wa dini 110, wazee wa mila 90, ngariba 38 na  waendesha bodaboda 361.
Uelewa mdogo wa wanafamilia na jamii kuhusu malezi yanayofaa kwa watoto na mbinu za kuimarisha mahusiano miongoni mwa wanafamilia huathiri ukuaji wa watoto na kupelekea watoto kukosa mahitaji muhimu katika familia na hatimaye kukimbia nyumbani. Kupitia kitini cha elimu ya malezi, familia zitaweza kuboresha malezi na familia kuendelea kuwa mahali salama panapofaa kuishi.

Kupitia Mpango Kazi wa Taifa wa Kutokomeza Ukatili Dhidi ya Wanawake na Watoto 2017/18 – 2021/22, Wizara imeunda vikundi vya malezi na kutoa elimu ya malezi katika familia 800 za mikoa ya Njombe, Iringa na Mbeya. Wizara itaendelea kuhamasisha uundaji wa vikundi katika mikoa mingine ili kuimarisha wajibu wa malezi katika familia.

Jamii imekuwa na mtazamo hasi kuhusu malezi  na hivyo kuongezeka kwa mmomonyoko wa maadili kwa watoto na vijana. Utamaduni wa familia tandaa kushirikiana katika malezi umekuwa ni changamoto kwa wakati huu kutokana na kukosa mwitikio wa uwajibikaji katika malezi ya wanafamilia katika jamii.

Matokeo yake baadhi ya watoto wa mekuwa wanajilea wenyewe pale wanapofiwa na wazazi, wazee nao wanakosa matunzo stahiki na wenye ulemavu wamekuwa wakitaarifiwa kufungiwa ndani. Wakati tunaadhimisha Siku ya Familia Duniani kwa mwaka 2018, wazazi na walezi wanatakiwa kuzingatia upendo na mahusiano mema ndani ya familia ili kujenga familia na jamii iliyo bora na yenye maadili.

Siku hii huadhimishwa na Nchi Wanachamawa Umoja wa Mataifa kwa mujibu wa Tamko Namba 47/237 la Umoja wa Mataifa la tarehe 20 Septemba, 1993. Kwamatinki hiyo madhumuni ya maadhimisho haya nikutambua umuhimu wa familia kama chanzo cha jamii. Kaulimbiu ya Maadhimisho ya mwaka huu ni “Malezi Jumuishi: Msingi wa Uzalendo, Utu na Maadili ya Familia na Taifa”.

Imetolewa na
Kitengo cha Mawasiliano Serikalini
Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto
(Idara Kuu ya Maendeleo ya Jamii)
13/05/2018

Share this article :

0 comments:

Post a Comment

 
MZUKA BLOG © Copyright 2014. All Rights Reserved.

Powered by MATERU FROM IBS.
imagem-logoRudi Juu